The Chant of Savant

Tuesday 5 April 2016

Kijiwe kwenda kunywa chai na Dk Makufuli


            Baada ya rahis Joni Kanywaji Makufuli kukikuna kijiwe pale alipotangaza kuwa anataka Bongo iondokane na uombaomba na kugeuzwa shamba la bibi, Kijiwe kinapanga kwenda kumpongeza na kumpa inshu nyingine tayari kwa utumbuzi.
            Mpemba anaingia akiwa na gazeti la Pashapasha. Analiweka mezani baada ya kuamkua na kusema, “Yakhe mmesikia maneno mazito ya rahis?”
            Kabla ya kuendelea Mbwamwitu anamuuliza, “Maneno yepi wakati rahis anasema mengi tu?”
            Mpemba anajibu, “Ama kweli mswahili ntu wa ajabu sana. Mie nauliza swali nawe wajibu kwa swali!”
Mbwamwitu anajibu, “Inategemea na swali ulilouliza. Kama umeuliza jibu unategemea nini zaidi ya swali”
            Mgosi Machungi anaamua kukamua mic, “Mie naona Ami hajakoshea sema ungesema hujampata vizui.”
            “Mgosi acha utani. Eti sikumpata vizuri siyo?”
Mpemba anakatua mic, “Wallahi hata mie sinjanpata Mbwamwitu vilivo vinginevo ningentosheleza tu. Maana uwezo ninao ati.”
            Mchunguliaji aliyekuwa akisoma gazeti anaamua kuwachomekea wenzake, “Mie wote nimewapata vizuri na nadhani sasa ngoja niwatosheleze. Nadhani Ami anamaanisha habari hii.” Anaonyesha gazeti na kichwa cha habari kinasema, “Rais kufyeka mishahara ya kijambazi kwenye mashirika ya umma.”
            Mijjinga aliyekuwa akingalia huku akitabasamu anakatua mic, “Hata mimi namuunga mkono Dk Kanywaji. Haiwezekani tuchape kazi wezi wachache wanufaike wakati sisi tukiumia kwa ukapa, ukata na ukwete. Hebu angalia hapa.” Anafunua gazeti na kusoma, “Ndugu zangu wana kaya, kuna gendaeka wanalipwa hadi madafu milioni 40.”
            Kapende anaamua kutia guu, “Huu kwangu ni ujambazi hata kama majambazi wanaoutenda wanatumia kalamu. Nadhanai hapa tunapaswa kurekebisha sheria ili majambazi hawa wa kalamu wahukumiwe na kupewa adhabu sawa na wale wanaotumia silaha hasa ikizingatiwa kuwa na kalamu ni silaha tena yenye nguvu kuliko bundiki. The pen is mightier than a gun.” Anamalizia kwa kimombo kiasi cha kuwaacha wengi hoi.
Kabla ya kuendelea Msomi Mkatatamaa anamua kumkosoa Kapende kwa kusema, “The pen is mightier than the sword. Hata hivyo hujakosea sana na hasa ikizingatiwa kuwa kiCameron siyo lugha ya kaya. Kama rahis mwenyewe wakati mwingine anachapia kwanini nasi tusimuunge mkono hata kama si jambo jema?”
            Kapende anajitete, “Nilifanya makusudi ili kuona wasomi wenzangu kama mtagundua. Asante sana kwa kunikosoa daktari wa falasafa mwenzangu.”
Msomi anaendelea, “Huyu jamaa kama atafanya kweli, ni kweli kuwa kaya yetu siyo maskini. Maana ukiangalia inavyoibiwa na kila nyani na kinyama mwitu chenye sura ya binadamu, unashangaa hata mantiki ya wanene wetu kwenda kujidhalilisha ughaibuni kubomu wakati mshiko umejaa hapa nyumbani.” Anakohoa kidogo na kubwia kahawa yake na kuendelea, “Kama gendaeka wachache wanajipendelea hivi, hivi tukitenda haki tukakomesha ufisadi sisi si kaya tajiri kweli? Juzi nilimsikia Dk Kanywaji akiwa Chato akisema kuwa waligundua kuwa kuliwa na wahalifu waliokuwa wakipokea mishahara 17. Hivi huyu naye anahitaji kupelekwa mahakamani na kupewa dhamana au kunyongwa right on the spot?”
            Mipawa anajibu, “Usemayo ya msingi. Kaya yetu si maskini bali ina umaskini wa kutengenezwa na gendaeka wenye madaraka wasiyojua kuyatumia kama jamaa yetu chekacheka bin Njaa Kaya. Umenikumbusha mambo yalivyokuwa yameharibika kiasi cha kaya kubakwa. Umeona yule miss alivyoburuzwa kwa pilato? Sisi tulidhani mchezo unaishia kwenye kujihonga na kuchaguliwa miss kumbe wenzetu wanatumia kila mwanya kutuibia njuluku! Hakuna jizi lililonichukiza kama Hass Kitilia. Haya magendaeka ni ya kutundika shaba kama wanavyofanya wenzetu wa Uchaina.” Anapiga chafya mara mbili na kuendelea, “Wana bahati wana hizaya hawa. Kama siyo pilato kuwanyima dhamana ningeenda mwenyewe kunyonga nyani tena hadharani bila kujali nini kitafuata.”
            Sofia Lion aka Kanungaembe anapunyua mic, “Kaka hata mimi sikuamini kuwa na mamiss wanaweza kuwa matapeli na majambazi. Ama kweli huyu mtoto wa kike katutia aibu akina mama wa kaya hii!”
            Kanji hangoji amalize. Anamchomekea mshikaji wake Sofi, “Acha Sofi mimi chomekea veve. Veve nasangaa hii miss kuwa tapeli! Mimi jua hii miss sana. Kwanza nakuwa na biasara na ile festi ledi Anna Kappa Tamaa. Kama chunguzi zuli nafanya, takuta na hii Ana Tamaa hata hii Salamia Kwetete iko dani ya hii vizi. Sasa tajua kama gongo iko juisi au nywaji.”
            Msomi anaamua kutia guu tena, “Nyinyi mnashangaa huu ujambazi? Kimsingi, hata huu ujambazi wa kutumia silaha umezalishwa na mfumo huu unaowalea majambazi wa kalamu. Napendekeza twende ikulu kupata chai na Dk Kanywaji halafu tumpe mbinu ya kukabiliana na ujambazi huu. Lazima tubadili sheria zetu za kushughulikia ujambazi uwe wa silaha au kalamu. Siku zote nasema turejeshe sheria za maadili kwa wanakaya wote. Kila mtu aeleze alivyochuma. Nadhani tukipambana na kero hisi kisayansi kwa kutumia sheria tutashinda badala ya kutegemezea usongo wa rahis peke yake.  Lazima tufanye mapinduzi kimfumo na siyo kutumia jazba na kulalamikalalamika.”
            Kijiwe kikiwa kinanoga si Dk Kanywaji akatutwangia na kututaka twende ikulu kupata chai na kubadilishana naye mawazo!
Chanzo: Tanzania Daima, Aprili 6, 2016.

No comments: