The Chant of Savant

Monday 29 June 2015

Wagombea CCM mtendeeni haki Kikwete


                   Imekuwa kama fasheni sasa. Kila mtangaza nia ya kutaka kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupeperusha bendera yake katika uchaguzi ujao, anamponda rais Jakaya Kikwete wanayenyukana kumrithi. Wanamuona kama mtu ambaye hana lake tena baada ya kutundika viatu mwishoni mwa mwezi wa kumi. Kila anayekuja anakuja na gea ile ile ya kufanya vyema kuliko Kikwete ambaye wanamuonyesha kama mtu wa hovyo, asiye na msimamo, mwoga na ambaye ameruhusu nchi ijiendee. Hawamtendei haki rafiki yao hata kama kweli ana udhaifu wake unaojulikana. Pia wanampomshambulia Kikwete bila kuushambulia mfumo uliomtengeneza, wanawandanganya wananchi. Kwani, bila kubadili mfumo jambazi wa sasa, hata akichaguliwa malaika ataondoka ikulu akiwa shetani. Huu ufisadi na ulegevu wanaomshambulia Kikwete kwao,licha ya kuushiriki, watautenda wakiingia madarakani. Kama tungekuwa na mfumo unaoshikisha adabu watawala baada ya kuondoka madarakani kwa kuwashitaki wanapofanya madudu, Kikwete sasa asingekuwa analaumiwa. Tuliyaona alipoondoka Benjamin Mkapa akiwa na tuhuma za kuiibia umma. Kesho atafuata Kikwete na kesho kutwa atafuata mmoja wa hawa wanaomuandama.
          Haiingii akilini watu wanaounda serikali ile ile kuitupia madongo wakati walikuwamo –na bado wengine wamo –ndani na walikuwa na uwezo wa kutoa ushauri au kurekebisha mambo kwa nafasi zao. Hata hivyo, wanaomshutumu Kikwete wakati walikuwa naye kitanda kimoja wana bahati. Angekuwa marehemu baba wa Taifa marehemu Mwl Julius Nyerere sina shaka. Angeishawafukuza wengi kazi ukiachia mbali kuwapaka kuhakikisha hawapenyi kwenye chujio la CCM. Washukuru Mungu CCM imeishiwa hata uongozi wenye kuweza kukaripia watovu wa nidhamu kama hawa. Hata hivyo, haimaanishi kuwa watu wasikosoe. Kinachopaswa kuzingatiwa ni kwanini wakosoe sasa wakati walikuwa humo humo wakitenda makosa wanayojifanya kukosoa sasa? Hii ni aina fulani ya unafiki unaonuka.
Kwa vile Kikwete amejigeuza punching bag –kwa sababu anazojua mojawapo ikiwa kuwamo ukweli kwenye madai ya wahusika –wanaweza kumtukana watakavyo na asifanye kitu kwa vile naye alipoingia aliingia kwa gea hii ya maisha bora kwa wote akinaanisha wakati ule maisha hayakuwa bora chini ya Mkapa. Ukimpiga mzazi wako nawe mwanao atakupiga tu. Inashangaza hata akina Salva Rweyemamu anaowalipa vizuri wafanye kazi ya kumtetea hawafanyi hivyo. Je nao wamemgeuka wakitafuta fursa ya kupata mwingine wa kuwatumia ili wamtumikie baadaye kama walivyofanya kwa Kikwete? Je hawa nao wanalipwa kwa kazi gani iwapo wanalala kwenye usukani?
          Makala hii hailengi kumtetea Kikwete. Hiyo ni kazi ya watajwa hapo juu hata kama hawaiwezi au kuigwaya kwa sababu ya maslahi binfsi baadaye. Tunachotaka kuweka wazi ni kwamba wananchi wasihadaike na kuwaona hawa wanaomkosoa au kufichua udhaifu wake ni tofauti naye. Ni wale wale. Jogoo wote hunya ndani kiasi cha kuwafundisha vifaranga. Wanachofanya ni utapeli wa kutaka waonekane wao ni safi wakati wamo kwenye dimbwi moja la matope liitwalo CCM. Kwa lugha nyingine ni kwamba anayeiponda serikali ya Kikwete akitokea mle licha ya kuwa moungo ni mnafiki ambaye anapaswa kuogopwa kuliko hata ukoma. Kwani, anajiponda mwenyewe au kujivua nguo akiadhani anamfanyia hivyo Kikwete. Kama ameweza kumgeuka huyo aliyemtengeneza atashindwa kuwageuka wananchi? Wanachosema kingekuwa na maana kama wangekuwa nje ya serikali husika tena baada ya kujitoa kupinga hicho wanachosema sasa. Waulize: Mlikwina au mlikuwa wapi?
          Ukisikia kauli kama hii iliyotolewa na waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Uhusiano wa Kimataifa Bernard Membe unashangaa. Membe alikaririwa akisema, Ninawatumia salamu mapema, sitakuwa na kigugumizi kwa wanaotesa Watanzania. Nitahakikisha Watanzania wanachukia rushwa na kutakuwa na sheria kali dhidi ya mtoa na mpokeaji rushwa. Kama ni watumishi wa umma, watakwenda na maji....” Je asemayo Membe ni ya kweli au funga kamba? Akiwa kama waziri alifanya nini kupigana na rushwa. Kama Membe alishindwa kupambana na rushwa kwenye wizara yake ambapo mabilioni ya shilingi yametumika kifisadi kwenye balozi zetu nje ataiweza nchi nzima?
          Mwingine aliyewaacha wengi hoi ni Samuel Sitta aliyekaririwa akisema, “Ili kukomesha tatizo la rushwa, hatuna budi kutunga sheria itakayotenganisha biashara na uongozi.” Ni ajabu anayesema haya ni mwanasheria na aliyewahi kuwa spika wa Bunge. Kwani Kikwete ndiye aliwazuia kutunga hiyo sheria au ni kamba kama kawaida ili uonekane una sera na mipango vya kuwakomboa wananchi wakati letu moja?
          January Makamba naye hakubaki nyuma kwenye kurusha madongo kwa serikali ya Kikwete aliyefanya kosa akamteua tokana na ushawishi wa baba yake. Sasa anamlipa ambavyo hakutegemewa. Alikaririwa akisema, “nitafanya mabadiliko ya kisheria, kimfumo, kitaasisi na kijamii ikiwamo kuipa meno Takukuru kuwa na mamlaka kisheria ya kuwashtaki watuhumiwa wa rushwa moja kwa moja mahakamani.” Hivi bila rushwa itokanayo na kujuana na kulipana fadhili Makamba angekuwa hapo alipo tokana na jina la baba yake?
          Mwingine aliyewaacha wengi hoi ni Stephen Wassira aliyekaririwa akisema, “Kumbukeni sijatajwa katika kashfa kama za Escrow, EPA, Richmond na nyinginezo.” Je aliyetajwa kwenye hizo kashfa zote zaidi ya rais Kikwete ni nani? Je kutotajwa kwenye EPA Escrow na Richmond ndiyo kigezo cha kuwa msafi wakati kuna kashfa nyingi zinapita bila kutangazwa wala kushughulikiwa?
          Tumalizie kwa kuwashauri wananchi hasa wapiga kura kuwa makini na waongo na wanafiki wanaofanya u-Petro wa kumkana Bwana na u-Yuda wa kumsaliti Bwana. Kambale wote wana sharubu na nyani wote mchezo wao ni mmoja. Hivyo, msiwaamini sana sana wakaange kwa mafuta yao kambale hawa.
Chanzo: Dira Juni 29, 2015.

2 comments:

Anonymous said...

Salamu Mwalimu Mhango,
Kama tunavyojua siasa ni mchezo mchafu kama mabingwa wa uchunguzi wa siasa wanavyosema,na hili linadhihirika hapa kuhusu CCM kupigania kwa kila njia kubaki madarakani kama walivyotuahidi kwamba watatuwala kwa miaka 50 ijayo.Hii tulionalo sasa hivi katika mbio hizi za kupigania tiketi ya kuwania kinyangányiro cha urais ni kama show tu ya Tom and Jerry,ukweli ni kwamba kupakwa maptope kwa Kikwete,kushutumiwa,kumpiga vijembe na blah blah blah zote hizo ni kuwafunika watanzania akili na macho (divert attention) ili akili zao na macho yao yashughulishwe sana na hawa wagombea kinyanga'anganyiro cha urais ndani ya CCM kuliko watanzania hao kuwashugulikia viongozi wa kambi ya upinzani na kujipanga na kujizatiti kuiangusha CCM na kuitoa madrakani, na kwa hili CCM wamefanikiwa.Swali linalojiuuliza hapa kwa nguvu ni hili kwani kuchukua hizo fomu za kugombea urais ndani ya CCM imekua ni kama kuchukua kadi za mwaliko wa sherehe za harusi?iweje mpaka usawa huu kuna zaidi ya wagombea 30 ndani ya CCM wengine hata hatuwajui walikuwa wapi ndani ya CCM hiyo lakini wameibuka from nowhere na kila mmoja wao kwa hamasa ya hali ya juu kabisa anadai kwamba anastahiki kuuvaa urais,sasa kama si kutuona sisi wananchi ni matahira ni nini basi?
Mwalimu Muhango,walimtukana,walimbeza,walimkosoa Kikwete kwa wenye akili akili tunajua tu kwamba ,mara hii kabla ya uchakachuaji wa kura zetu wameanza na uchakachuaji wa akili na macho yetu kwa hiyo watanzania shughuli inayotushughulisha ni kuwasoma na kuwachambua wagombea hao zaidi ya 30 kana kwamba uchaguzi ni wa chama kimoja.Mwalimu Mhango,kadhia sio kumkana au kumsaliti Bwana wote hao ni timu moja na ndio wale wale wale.Kwa hiyo hakuna sababu ya wananchi kupoteza wakati wao kwa kuwashughulikia, kuwafuatilizia na kuwachambua majambazi,wanafiki,waongo na mafisadi wa level ya juu ya nani atakuwa Rais mtarajiwa kana kwamba hakuna hapo kambi ya upinzani.Ni show tu hiyo ya Tom and Jerry tuwe na hadhari vinginevyo tumeumia.

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Anon nisingependa kuongeza kitu kwenye nasaha zao kwa watanzania kuwa hawa jamaa ni karata tatu. Unaodhani ni wachezaji kumbe ni mtapeli wale wale wanaotaka kukuviti kwenye mkenge wao. Kimsingi nami naona kama lao ni moja.
Hivyo, muhimu wananchi kuustukia huu mkakati wa kuwachakachua kiakili. Nimependa analogue yako.