The Chant of Savant

Tuesday 9 June 2015

Kijiwe chafurahia mipasho ya watangaza nia ya urahis



          Baada ya songombwingo na kila aina ya ngurumbili kutangaza nia ya kuwania ulaji wa dezo na rahisi yaani urahis, Kijiwe –kwa furaha –kimekaa kama kamati na kudurusu mtifuano na mshike mshike huu wenye kila aina ya patashika kasheshe, vitimbwi na mitimbwiriko.
          Mpembe anaingia akiwa na gazeti la Toboa. Anaamkua na kumwaga mada mezani. “Yakhe mmesikia hii mipasho ya wasaka urahis na ulaji wa dezo?”
          Kapende anadakia, “Hawana lolote hawa. wengi mafisadi wa kunuka japo wanajifanya wana sera za kutukomboa wakati moyoni wana mipango ya kutuangamiza kama hawa wanaoondoka.”
          Mbwamwitu anachomekea, “Wengi viherehere kama alivyosema mwana wa Mchonga japo naye hafai.”
          “Wengine wanafuata mkumbo ukiachia mbali kutengeneza mazingira ya kutaka wawemo kwenye ulaji kama mmoja wao atapenya. Nionavyo mwaka huu hapenyi mtu. Maana kwa wanavyochafuana lazima wapingaji wachuke waweke waa kama watakuwa makini kutumia huu mtifuano.” Anasema Mijjinga huku akibwia kahawa yake.
          Mgosi anatia timu kwa chati, “Hakuna sehemu wameniacha hoi kama yule  Kimbelembele Mwehujuu Michembe kusema eti atativusha. Kumbe timekwama bahaini. Ina maana huyu dogo anakii kuwa Njaa Kaya ametizamisha? Makubwa haya wagosi tate nane tate nane.”
          Msomi Mkatatamaa aliyekuwa akibofya ki-Samsung Galaxy 5 anaamua kula mic, “Wote wamepayuka hakuna aliyeniacha hoi kama Freddie Sumayi aliyekumbuka blanketi wakati kumekucha. Eti anasema kuwa Chama Cha Maulaji kikipitisha fisadi atajitoa. Mbona amechelewa. Kama chama chenyewe ni genge la mafisadi anategemea huyu msafi kitampata wapi.”
          Kabla ya kuendelea mheshimiwa Bwege anamchomekea, “Naona huyu buda anaweweseka hasa ikizingatiwa kuwa hawezi kupenya kutokana na kuwa na kashfa ya kuuza nyumba za wachovu wakati wa utawala wake na Chinga Dugong Ben Makapi. Kama anataka kufanya kweli angeishajitoa zamani gani! hata hivyo, sishangai. Hawa ni wanasiasa ambao –mara nyingi –huwa hawana tofauti na vyangu kimaadili na madili.”
          Msomi anaendelea, “Hakuna aliyeniacha hoi kama profwedheha Muongo kusema eti ataongoza kaya kisayansi. Sijui alisahau kusema kifisadi au kiescrow akasema kisayansi? Huyu kama kuna kinachomfaa si kingine bali kwenda kwa bosi wake Jimmy Lugemalayer na Singasinga wakamtumie kule.”
          Kanji anadandia, “Kama yeye kwenda escrow tumia yeye si tapata aibu? Veve sema witu zito sana Somi. Ile yote nashiriki escrow hapana paswa gombea rahis jamani.”
          Sofia Lion aka Kanungaembe aliyekuwa na usongo wa kuchangia anakula mic, “Jamani tunapaswa kuwa makini tunapotoa shutuma. Hivi kuna mtu ana ushahidi dhidi ya mheshimiwa huyu au fitina na chuki binafsi?”
          Msomi hangoji mwingine ajibu. Anakula mic huku akitabasamu na kumwangalia Sofi kama kwa dharau hivi na kusema, “Da Sofi unataka ushahidi gani? kwani alifukuzwa ulaji kwa sababu gani na kwanini? Je huu si ushahidi tosha sawa na ule uliomfukuzisha Eddie Luwasha ambaye kwenye kigwena chake aligwaya kugusia Richmonduli akidhani sisi tutasahau?”
          Inaonekana Sofi kashikwa sehemu nyeti. Kwani badala ya kutoa macho na kunung’una hajibu maswali ya Msomi.
          Mpemba anarejea,”Wallahi usemayo Nsomi mazito kweli kweli. Hawa wajalaana wadhani sisi mataahira na wasahaulifu kiasi cha kujitiatia na kujiletaleta eti tuwape ulaji watuuze zaidi?”
          Mzee Maneno anachomekea, “Ami eti wanajitiatia na kujiletaleta? Au ndicho hicho kimbelembele cha vidokozi anachosema Makorongo Mchonga?”
          Mipawa anatia timu, “Wajameni mwashangaaga kusikia hii mipasho. Hamjui kuwa wakati waliozoea kula wenzao kuliwa umefika? Watabwabwaja mengi na kuvuana nguo sana tu. Nadhani laana ya kukwanyua njuluku za wachovu inaanza kuwaandama kiasi cha kumalizana wao kwa wao. Hatuna haja ya kusherekea anguko hili la ghafla la genge la mafisadi.” Sofi anamkata jicho la chuki lakini hasemi kitu.
          Msomi anarejea, “Usemayo mheshimiwa Mipawa ni kweli tupu. Hamuoni wanavyoanza kugeukana kiasi cha wale waliojidai ni marafiki wa mtukufu tena si wa kukutana barabarani wanavyolialia kama vichanga? Huoni kila mmoja anavyojitahidi kumtupia Njaa Kaya mzigo wakati walikula na kuvurunda wote. Namuonea huruma rafiki yangu Njaa Kaya ambaye alionywa kuwa ufisadi haulipi akaendeleza urafiki. Usishangae wakabwagwa na jamaa wakaishia lupango kutokana na ujambazi na ufisadi waliotenda. Hakuna aliyeniacha hoi kama Makorongo kutaja kabisa kuwa kuna wajaalaana wana mahekalu Dubai na kwingineko. Nadhani kazi sasa ni kwa wapingaji kupeleka ukweli huu mchungu kwa wachovu vijijini. Nadhani kilichoikuta Kanu kule kaya ya nyayo kinainyemelea CcM. Nadhani tuombe Mungu wazidi kuvuana nguo na kujitiatia kujua ili umma ustuke na kuwapiga chini.”
          Mbwamwitu anachomekea kwa utani, “Eti wanavuana nguo na kujitiatia! Ama kweli mmewachoka jamaa hawa!”
          Msomi anarejea, “Jamani haya si maneno yangu. Ni maneno ya Makorongo Mchonga aliyesema kuwa wengine wana kimbelembele na kiherehere asijue ni wote. Hivi ulitegemea nini jitu kama Dume la Nyani Steve Wahasira kutia timu wakati hana jipya wala lolote au kitegemezi cha Mgosi na huyu tabibu Kingwalangwala? Acha wapigane ngwala na kuchimbiana mikwara huku wakivuana nguo na kumwaga mtama kwa kuku tufaidi.” Anamgeukia Sofi na kuuliza, “Mbona akina mama hawatii guu au wanaogopa kuvuliwa nguo? Ama kweli vita ya kunguru ni neema ya panzi kama watakuwa makini.”
          Kijiwe kikiwa kinaendelea si ukapita msafara wa watangaza nia wakitaka kutoana mcho. Acha tuwashangae na kuwashangilia tukiomba waendelee kutupa uhondo!
Chanzo; Tanzania Daima Juni 10, 2015.

No comments: