The Chant of Savant

Wednesday 30 October 2013

Corruption: Will Joyce Banda Fire Herself?

 
News that Malawi female president Joyce Banda dissolved her cabinet spread like bush fire. Banda had to swallow a bitter pill after it came to light that her government was either ignoring or condoning malpractices. It was sleeping on the wheel.
 Banda stole thunder earlier last year, after the death of Bingu wa Mutharika whose courtiers and stooges wanted to stop the then vice president Banda from taking the oath of president as Malawi constitution stipulates. The move by Mutharika’s inner circle was opposed by many in Malawi and abroad. Abhorring such undemocratic move, Malawians threw their support behind Banda believing she’d reverse economic limbo Malawi was in.  The coming of Banda into the big picture was expected to bring breath of fresh air. However, things didn’t work as Malawians expected. After ascending to power, Banda proved to be more a disaster than her predecessor. Instead of addressing the very problems Malawians faced, she embarked on vengeance, fuata nyayo and knockdown policy aiming at punishing Mutharika’s inner circle that’s replaced by her own cronies. She went ahead devaluing Malawi Kwacha to begin with. Thereafter, fissures in Banda regime started to surface after being accused of nepotism and corruption. Things went from bad to worse and corruption became rife.  All of the sudden, the woman who used to convince Malawians that she’s a mother who would care about them became another monster. It as if Malawians were afraid of a lizard to death to end up embracing a gator.
 Again, tongues didn’t stop waging especially for those in the know regarding what has been going on in Malawi.  After firing the cabinet her supporters started singing praises to their heroine for ‘taking’ on the vestiges of corruption little knowing that she was acted on orders from above. Detractors did not jump into praise-singing bandwagon. They are asking: Why taking dissolving the cabinet after being lectured by donor community? Detractors have a point. Recently the EU warned Banda to put her house in order.  Alexander Baum, the Head of EU Malawi mission was quoted as saying, “There is need for a cleanup before we make our disbursement.”  Pressure on Banda was exerted after top finance ministry official, Paul Mphwiyo, who’s seen as an anti-corruption crusader, was shot and wounded last month.
The shooting of Mphwiyo provoke the blow up of many especially anti-graft campaigners who termed it as a move to silence Mphwiyo. Many wondered how Malawi would be ripped off by a few venal officials while the government was just doing nothing. Baum added, “All this massive looting was happening under the nose of auditor general’s office and malpractice was not detected or discovered.” although Baum did not directly implicate the government, his harsh words aimed at sending the message which Banda got and acted on it.
Looking at the mess Malawi is in under a female president, the whole belief that females are less corrupt than men as it has always been drummed in up does not hold water especially in Africa.  The thing is. For Africa females and males are equally corrupt and unpredictable. Refer to the scam involving another female Liberian president whose children are in high offices undeservedly. The situation in Liberia became worse so as to force madam president to fire her sons in order to save her face.
More on Banda, last year her minister of justice who also is attorney general Raphael Kasambara admitted to have spent public money without following proper procedure. He was not fired despite admitting wrong doing. Was Banda waiting for? Did Kasamabara firing need EU’s pressure?  Kasambara’s case is but a drop in the ocean of Banda’s administration regarding graft. Banda was required recently declare her wealth as a step towards combating graft. Sadly though, Banda refused to do so. Can such a person be clean? Leading is always to be in front of others and lead by deeds not mere words.
Again, many are still asking. If Banda seriously aims at dealing with the vestiges of corruption, then when will she fire herself given that she is the core and pillar of corruption in Malawi currently? Ironically, what was drummed as reshuffle wasn’t. Instead, Banda recycled the same kit and caboodle of courtiers.
Source: The African Executive Magazine Oct., 30, 2013.

Walioficha pesa Uswazi wachomwe au wanyongwe

 
BAADA ya kugundua kuwa kuna mchezo mchafu wa kuwachukulia wachovu kama mataahira huku wahusika wakizidi kuiba njuluku zao, kijiwe kimekuja na suluhisho la kudumu.
Mipawa analianzisha, “Nimecheka kusikia kuwa dokta Eddie Hoshea na Mura Freddie Weelema nao ni wajumbe wa kamati ya kufuatilia njuluku iliyofichwa Uswizi.
“Yaani unampa mbwa kazi ya kulinda nyama halafu unategemea kuwepo nyama au mifupa?”
Kapende anachomekea, “Hizi nazo ni sanaa na ngonjera ambazo wanasiasa watatumia kujipatia kura ya kula na ujiko kama anavyofanya Mzito Kabwela ambaye alituahidi kutaja lakini akawa anajikanyaga kama Dokta Mwakiwembe na wauza bwimbwi.
“Kwa nini msifunge madomo yenu na kutafuta mbinu nyingine ya kupata ulaji badala ya kutugeuza majuha wakati sisi siyo?”
Kapende anaamua kupasua jipu. Anasema, “Mimi sasa nataja potelea mbali liwalo na liwe.
“Walioficha njuluku Uswisi wanajulikana. Leo mie nataja. Nambari wani ni Endelea Chengaaa, Idiiliishua Rashidu, Niziro Kadamage, Rahasttamu L’ Aziz, Billy Ngeleza, Mood Daweje aka bilionea toka kaya kapuku, Pitia Noni, Eddie Ewassa, Njaa Kaya, Bazil Pesatatu Mrambaramba, Ben Dugong Makapu na nkewe na Dan son of Johah.”
Wakati tukiendelea kusuburi ataje zaidi si akamalizia kwa kusema, “Wengine nitawataja next time.”
Pamoja na kutuacha kwenye suspense Kijiwe kinamshangilia kwa hoi hoi na nderemo angalau kwa kuthubutu kutaja huku kikisema, “Wanyongwe au wachomwe moto kama vibaka.”
Kelele zimehanikiza hadi wapita njia wanaopenda kushangaashangaa wanasimama na kushangaa. Bahati yetu wakati watu wakitushangaa bila kujishangaa hakuna ndata aliyepita.
Maana, wanavyopenda kujitiatia asingesita kuuliza kunani.
Baada ya kijiwe kutulia Mipawa anasema, “Umemsahau Kanji?” Anasema kwa utani huku akikamua kombe lake la tangawizi.
Maana leo zimemtembelea kiasi cha kuachana na kahawa na kunywa tangawizi.  Mwisho wa mwezi huu ati.
Kanji kashikwa pabaya. Anajitetea, “Mimi iko clean. Haina pesa kule Swizz. Kama napata pesa kuba kama hiyo kwa nini hapana hamia London bwana?”
“Kanji usitifanye majuha nawe. Kwani wote walioficha njuuku Uswisi lazima wahamie London?
“Ingekuwa hivyo mbona kina Ostam L’Aziz wangeishaishia London kama siyo Iani (Iran)?” anang’aka Mgosi Machungi huku akimtazama Kanji kwa dharau ya kisambaa.
Msomi aliyekuwa kimya akishangaa jinsi wanywa kahawa walivyoamka anaamua kutia guu, “Hakuna kitu kinanisononesha kama kushuhudia wanakaya tukikaa na kuangalia wakati tukiibiwa kila uchao kana kwamba hii pesa si yetu. Kitaalamu tunasema kuwa ‘power is always fluid. Like water, even air, it can move from one hand to another’.
“Kimsingi mali tunayo tunaikalia.  Jamani tuamke na kuhakikisha tunazuia ujambazi huu wa mchana vinginevyo tutaliwa kila mara.”
Mzee Kidevu anaamua kumkumbushia itifaki. “Msomi taratibu, kumbuka itifaki Kikameruni hicho kaka.”
Mipawa na Mijjinga wananong’ona kitu kuhusiana na mzee Kidevu kuchukia Kikameruni wakati akikumbatia Kiarabu.
Mzee Kidevu anasema, “Eti mali tunayo tunaikalia? Tuombe msamaha Msomi.”
“Msomi umesema vyema. Mimi si maskini. Nimesikitishwa na hawa wezi. Hebu fikiria. Ushoto tunazalisha matunda na yanaoza.
“Hatina kiwanda hata kimoja. Je, huku si kutifanya maskini bila sababu yoyote zaidi ya upofu na ulafi?
“Hivi hii njuluku ingetiwezesha kujenga viwanda au mashule hata baabaa ngapi?” Machungi anazoza.
Anaendelea, “Tiamue. Tiende huko mawizaani. Tiwakamate na tiwafukuze wanaotiibia kila siku kana kwamba tu mataahia au vipofu. This is too much.”
Bi Sofi Kanungaembe ambaye hivi karibuni alilizusha kule kwa kina Twambombo anakwanyua mic, “Siungi mkono utoroshaji wa fedha za umma. Ila ningeshauri tumpe muda mtukufu rais afanye uchunguzi na achukue hatua.”
Mijinga anaamua kukatua mic, “Bi Sofi acha nikuingilie.”
Kabla ya kuendelea Mbwa Mwitu anamuonya, “Chonde chonde Mijjinga unataka umuingilie bibi wa watu kwa kosa lipi?”
Kijiwe hakina mbavu kwa jinsi Mbwamwitu anavyotafsiri vibaya kusudio la Mijjinga. Anyway, ndiyo Kiswahili chenyewe. Unasema hili wanafikiri lile.
Mijjinga anajitetea, “Basi ngoja nidandie.”
Kabla ya kuendelea Mpemba anasema, “Loo umeona kuingilia haitoshi sasa waamua dandia ami!”
Mijjinga anapuuzia utani na kusema, “Sasa unazidi kuniudhi. Rais achukue hatua ya nini iwapo serikali yake imekalia kashfa hii kwa miaka yote? Umesahau EPA mara hii! Hujui kuwa nyingi ya fedha iliyofichwa nje inatokana na MaEPA na Ma Richmonduli Kagoda na Meremeta rada na ndege mkangafu ya rais?”
Machungi anadakia, “Mijjinga usitikumbushe hiyo EPA ambayo ni mahepe. Huoni yale majambazi ya EPA yanaitwa watukufu na majina mengine makubwa. Hivi sisi timeogwa na nani?”
Kabla ya kuendelea Mbwa Mwitu anachomekea, “Sisi hatujalogwa. Umelogwa wewe ambaye bila kumpiga mtu zongo hakukaliki.
“Dog Mwitu tiheshimiane ohooo! Wewe mtoto mdogo ambaye timecheza na mama yako inawezaje kusema eti timeogwa? Au unataka tikupige zongo la ukweli? Sema tikushughuikie sasa hivi.”
Mbwa Mwitu kuona yamekuwa hayo anaamua kujitetea, “Mgosi ndugu yangu hutaniwi?” Mpemba ambaye alikuwa kimya muda mrefu akisoma habari za Mzito Kabwela kutibua dili la majambazi wanono anampa gazeti Mchunguliaji na kukamua mic, “Yakhe mie nimekaa kimya nda nrefu. Sasa acha nipitishe fatwa wallahi. Mie naona tuache kulalama. Kama alivyosema Mgosi, twende huko maofisini tuwahukumu hawa wezi wanaojiona wana mamlaka juu ya kila kitu na kila mtu wakati mwenye mamlaka ni Subhana Wa Taala mwenyewe. Twangojani wakati kila kitu chaliwa? Mwataka nasi tuliwe?”
Kabla ya kumaliza Mgosi Machungi anachomekea, “Mgosi usitiletee mambo ya popo bawa hapa ohoo!” Mpemba anajihami, “Hapa mie sifanyi utani yakhe. Mambo ya popobawa yeshapitwa na wakati na waliofanyiwa ushenzi si mwawaona wakiumbuka wengine kupofuka?”
“Du bado hujamsahau Kamandoo wenu ambaye siku hizi ni apeche alolo huku akionekana kusononeka kwa aibu kutokana na ujinga aliofanya!” anachomekea Mijjinga.
Kijiwe kikiwa ndiyo kinanoga si likapita shangingi lililokuwa limembeba Mgimua.
Kila mtu alichukua kikombe chake na kuanza kulimwagia kahawa huku akilirushia kashata na tangawizi huku tukisema, “Acha siasa na ngonjera rejesha pesa yetu mliyoiba na kuficha Uswasi.”
Chanzo: Tanzania Daima Okt., 30, 2013.

Kikwete akiamua anaweza kuondoka shujaa




RAIS  Jakaya Kikwete, ingawa  wapo wanaomuona kama dhaifu tangu aingie madarakani, anaweza kubadili mwelekeo wa mambo na kuwa shujaa. Anaweza kufanya hivyo kama atafanya yafuatayo.
Mosi, kukiacha Chama Cha Mapinduzi (CCM) kijifie kutokana na kuishiwa kulhali. Anaweza kufanya kama alivyofanya rais wa mwisho wa lililokuwa Shirikisho la Kisoviet la Urusi, Michael Gorbachev. 
Pia anaweza kufanya kama rais wa zamani wa Romania, Ion Iliescu aliyekataa kuunga mkono uimla na umwagaji wa damu wa imla wa zamani wa Romania, Nicolae Causescu.
Pili, anaweza kufuta kile wakosoaji wake wanachoona kama ni makosa kwa kubadili aina yake ya utawala. 
Ingawa amebakiza muda mfupi madarakani, anaweza kuamua kuweka mfumo na mazingira ya watakaofuatia kurekebisha makosa ambayo mengi aliyarithi toka kwa mtangulizi wake aliyeiuza nchi kwa wawekezaji uchwara huku akihujumu kila rasilimali ya Taifa.
Tatu, anaweza kuendelea kuiandaa CCM kisaikolojia tayari kukabidhi madaraka kwa wengine wenye uwezo na kukubalika kwa wananchi.
Nne, anaweza kuachana na kile ambacho wakosoaji huita kuwafumbia mafisadi macho chini ya dhana mbovu ya ‘huyu ni mwenzetu’ ambayo kimsingi ndiyo imetufikisha hapa tulipo.
Tano, Kikwete anaweza kutumia mbinu mbadala ya kulibadili Taifa kwa kufanya mabadiliko kwa njia ya kupinga na kukataa mazoea ya kutawala kwa kuegemea kwenye maamuzi ya chama ambayo ndiyo silaha kubwa ya CCM.
Sita, anaweza kuangalia utaifa zaidi ya ukereketwa wa chama kama ambavyo imekuwa siku zote ambapo watu hufanya madudu na kutenda jinai kwa kisingizio cha kulinda maslahi ya chama. Rejea kwa mfano kuhusishwa kwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba na makosa ya kigaidi kwa kubambikizia wenzake makosa anayotenda.
Saba, anaweza kuamua kupingana na makada wote waliomzunguka wakimshawishi aendeleze uhohehahe kisiasa ili kuinufaisha CCM ambayo kimsingi ilishachokwa na Watanzania kutokana na kuendelea kuwazamisha.
Nane, anaweza kutumia miaka miwili iliyobaki ya kuwa madarakani kufanya yote mazuri na ya lazima aliyoacha kufanya kwa miaka nane iliyopita.
Tisa, anaweza kuanza kuandika historia mpya ya urais wake kwa kuendelea na mageuzi ya kweli ya kisiasa badala ya maigizo na sanaa za CCM. Mfano, anaweza kuzuia CCM kuendelea kuamrisha tume ya uchaguzi wakati wa uchaguzi kama ilivyotokea kwenye uchaguzi mkuu uliopita ambapo baadhi ya wabunge walioshindwa waliidhinishwa kwa mtutu wa bunduki.
Kumi, kwa vile ameishawaambia wazi CCM kujiandaa kisaikolojia, anapaswa kuendelea kuwaandaa akipangua wale wote wenye mawazo mgando na kufanya yale ambayo wasingetaka yafanyike kwa vile yatakiumiza chama.
Kwa mfano, anaweza kuamua kupambana na ufisadi, ujambazi, rushwa, matumizi mabaya ya fedha za umma, kutowajibika kwa watendaji wa umma. Kwa mfano, Kikwete anaweza kuanzisha vita dhidi ya wezi wa pesa za umma ambao wizi wao huripotiwa karibu kila mwaka na mdhibiti na mkaguzi mkuu wa Hesabu za serikali (CAG). 
Anaweza kuibadili Tanzania toka kwenye kuwa shamba la bibi na kuwa mali ya Watanzania ikiwanufaisha badala ya kunufaisha genge la watu wachache wanaotumia chama kushika hatamu kuliangamiza Taifa.
Anaweza kuachana na mfumo wa kujuana na kulipana fadhila. Kama ni kulipa fadhila, nadhani alizokwishalipa na aliowalipa wanatosha.
Kwa vile Kikwete haruhusiwi kugombea urais tena kisheria, hana cha kupoteza bali kufaidika kwa kuleta mapinduzi tena ndani ya kipindi kifupi. Hili linawezekana, linamfaa na asipoteze fursa hii ambayo Waingereza huita golden chance.
Kikwete si mjinga kiasi ambacho wale wanaomdanganya wanamdhania. Anajua fika kuwa kuna maisha baada ya kutoka Ikulu. Ameona wazi jinsi mtangulizi wake asivyo na heshima wala mashiko kwenye jamii ya Watanzania. Amesikia, kuona hata kusoma jinsi wachambuzi wanavyomtumia mtangulizi wake kama kielelezo cha maovu hasa yatokanayo na ufisadi. 
Rejea jinsi mtangulizi wake alivyoandamwa na jinamizi la kuua NBC, kujitwalia mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, kufanya biashara akiwa Ikulu, kuruhusu mkewe atumie Ikulu kuunda NGO ya ulaji, kuruhusu uingiwaji mikataba ya kiwizi ya uwekezaji ambao umegeuka uchukuaji na mengine mengi.
Pia Kikwete anajua kuwa Watanzania si wasahaulifu kama CCM ambavyo imekuwa ikifanya makosa na kuwachukulia. Tutoe mfano wa mbali kidogo. Nani, kwa mfano, amesahau kashfa iliyokabili utawala wa rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi ya Loliondo?
Kikwete anafahamu fika kuwa kila lenye mwanzo lina mwisho. Amesoma na kushuhudia historia ya maanguko la vyama kama UNIP (Zambia), KANU (Kenya), MCP (Malawi), NP (Afrika Kusini) na vingine vingi barani Afrika. Ameona machungu ya marais wa zamani hasa wale waliojisahau wakaendesha nchi kama mali binafsi na mali ya vyama vyao. 
Anajua yaliyowapata akina Fredrick Chiluba, misukosuko ya Bakili Muluzi, Laurent Gbago, Hosni Mubarak, Muammar Gaddafi, Zein ElAbedeen Ben Ali na wengine watakaofuatia ambao asingependa awe miongoni mwao. Kama kusoma alama za nyakati basi ndiko huku. Kufanya hivyo humkomboa mhusika na kumpa hakikisho la nafasi katika historia ya Taifa.
Tuhitimishe kwa kuendelea kumpa moyo na changamoto Kikwete asijipeleke mwenyewe majilini wakati ana njia ya kuachia madaraka na kuacha historia ya maana kwake. 
Sidhani kama Kikwete hayajui yote haya wala kama angependa awe muathirka wa mambo ambayo anayajua fika. Sidhani. Afahamu kuwa ataendelea kuishi baada ya urais. 
Pia afahamu kuwa mambo huenda yakibadilika. Yeye aliweza kumkingia kifua Mkapa jambo ambalo limembebesha lawama kwa kusema muache mzee Mkapa apumzike. 
Je ana uhakika gani kama atakayekuja atamkingia kifua wakati mazingira ya kufanya hivyo yanazidi kutoweka kutokana na hamu ya kuwa na Katiba Mpya ambayo ni zao la mabadiliko ya kifikra ya Kikwete? 
Afahamu kuwa kubadili katiba kutampa utajo katika historia ya Taifa na kuwa baba wa katiba na mabadiliko vinavyoweza kunusuru Taifa letu. Hakika Kikwete ana sababu ya kuchagua kumaliza urais wake akiwa shujaa na si mtuhumiwa wa matumizi mabaya ya uongozi. 
Akifanya hivyo, Watanzania watamsamehe makosa yake yote na kuanza ukurasa upya. Kwani naye ni binadamu. Ila asipofanya hivyo, ajue atakuwa rais mstaafu mwenye wingi shaka na misukosuko.

Chanzo: Dira ya Mtanzania Oktoba 2013.

Rais Kikwete watimue Chikawe na Wassira






MAWAZIRI  Mathias Chikawe (Sheria na Katiba) na Stephen Wassira ( Waziri wa Nchi Ofisi ya rais Mahusiano na Uratibu) ni watu wasioisha vituko. Alijua kuwa waziri Wassira angewaambia wapinzani kuwa wanalilia kwenda Ikulu kunywa juisi kana kwamba juisi ni kitu kikubwa? Inashangaza mtu mzima kiumri na mwenye madaraka kuhangaishwa na udohoudoho namna hii.
Naye Chikawe alitoa mpya aliposema kuwa atamshangaa rais Jakaya Kikwete kama hatasaini muswada wa katiba uliochakachuliwa. Hivi karibuni Chikawe alikaririwa akisema, “Nitamshangaa sana Rais Kikwete kama atashindwa kusaini muswada huo kwa sababu ya kelele za wapinzani.” 
Hakuna anayejua kigezo alichotumia kiasi kuonekana kama anamfanya rais mjinga kiasi hiki. 
Rais hawezi kusaini au kutosaini muswada kwa kuogopa watu wasimshangae. Kinachomsukuma rais kusaini au kutosaini muswada ni sheria. 
Naye Wassira alikaririwa akisema, “Hawa tumewalea siku nyingi na sasa wanafanya mazoea, ninachotaka kuwaeleza wasitarajie tena kuitwa Ikulu.” Kama tutauangalia ukweli bila makengeza na miwani ya mbao, kati ya wapinzani na Wassira nani amefugwa? 
Kuna dhana kuwa Wassira alikuwa akijitahidi kuwashambulia wapinzani ambako alitokea ili aonekane kuwa hana uhusiano nao tena. 
Wengi wanadhani kuwa Wassira anaiandama Chadema kwa maslahi yake yaani aonekane hana uhusiano nao tena ingawa kwa wanasiasa lolote linawezekana.  Kinachoshangaza ni ile ya Wassira kuwaandama wapinzani utadhani yeye hajawahi kuwa mpinzani. Ama kweli ‘nyani haoni kundule’.  Wakati mwingine ya nyani kutoona nonihino lake inaweza kutafisriwa kama unafiki au uchangudoa wa kisiasa.  
Ila ni vizuri Wassira na wenye mawazo kufu na mfu kama yake wakafahamu kuwa si wapinzani wote wako kwenye upinzani kwa ajili ya kukidhi tamaa na njaa zao. 
Wapo ambao ni makini na wana nia ya kuleta mabadiliko kwa Taifa lao. Mambo huenda yakibadilika.  
Hata hivyo Wassira anapaswa kuelewa kuwa wapo wapinzani walioko ndani ya chama kama yeye. Ila si vizuri kudhani wote ni kama yeye. Nani kwa mfano alijua kuwa Augustino Lyatonga Mrema au Maalim Seif Sharif Hamad wangekuwa na uswahiba na CCM?
Kinachofanya watu tuwashangae watu kama Chikawe wanaomshangaa rais kwa kukataa muswada uliochakachuliwa ni ile hali ya kuwa wanasheria wasiojua sheria. Inashangaza sana kuona mtu kama Chikawe waziri wa sheria na mwanasheria kitaaluma kufikiri kisiasa badala ya kitaaluma. 
Inashangaza kuona watu wanaopaswa kulinda katiba kama Chikawe ndiyo hao hao wanaotaka ichezewe na kila kundi la wahuni eti kwa vile ni wenzao. Nchi yetu haiwezi kuendeshwa kama kikundi cha ngoma ya mdundiko au baa ambapo kila mtu hujifanyia atakavyo. 
Hatuwezi kuwa wote vipofu tukiachia hatima ya nchi yetu kwenye sera za ubabaishaji na utendaji wa ajabu ajabu kama wabunge kukubali kutumiwa kuchakachua muswada ambao kimsingi ungewaletea ukombozi kama Taifa.  Isitoshe, suala la kujua kuwa muswada wa Katiba Mpya umechakachuliwa halihitaji kuwa na shahada ya sheria bali akili ya kawaida, ‘common sense’.  
Kuna wakati watu wanashangaa watu kama hawa waliteuliwa vipi wakati wanaonyesha kukosa uelewa mdogo ukiachia mbali ujuzi wa kuweza kuwa mawaziri. Tunajua kuwa wengine wamesoma tena nje kiasi cha kufikia kuwa na ‘Masters degree’. 
Je ni kwanini matendo na matamshi yao hayafanani na elimu wanayodai kuwa nayo au ni yale ya kutumia majina ya vyuo vya nje kuonyesha wana sifa kama siyo kughushi au kununua shahada za kwenye mtandao.
Kinachofanya watu wawashangae zaidi mawaziri hawa ni kuongelea mambo yasiyolingana na umri na nyadhifa zao ukiachia mbali mambo yenyewe kutoingia akilini. 
Kwa mfano, Ikulu na juisi wapi na wapi au kumshanga mtu anayefanya jambo ambalo ni la maana?  
Kuna haja ya mawaziri wetu kujitofautisha na wapiga debe, wavuta bangi, waimbaji taarabu au ‘rap’ au machinga wa pale mtaa wa Kongo. Kushindwa kufanya hivyo hupelekea watu kuamini kuwa wahusika wamefilisika kisiasa.
Kwa mawaziri kushindwa kutenda kama nyadhifa zao zinavyowatuma na ukiachia mbali kujiaibisha wao na bosi wao, wengi wanadhani wakati wa rais Kikwete kuwatimua ili kulinda heshima yake na Serikali ni sasa. Haiwezekani Serikali kuendelea kuwavumilia wahuni ikashindwa kuonekana ya kihuni kama wao. 
Maana Waingereza husema, nionyeshe marafiki zako nikwambie wewe ni nani. 
Hatuamini kuwa Serikali yetu na rais wake wamefikia kiwango hiki cha huruma na hasara. Hatuamini kuwa akina Chikawe na Wassira ni watu wanaopaswa kuonyeshwa iwapo mtu atamtaka rais Kikwete aonyeshe wenzake aambiwe yeye ni nani.
Tumalize, kwa kumtaka rais Kikwete asiishie kuwashangaa na kuwavumilia akina Chikawe na Wassira. 
Badala yake awawajibishe ili kulinda hadhi yake. Inabidi awaonyeshe kuwa yeye kuamuru katiba iandikwe upya hakuwa anataka kujiridhisha wala kufanya majaribio bali aliona hatima ya Taifa. 
Pia akina Chikawe na Wassira wanaomshangaa rais kwa kutimiza wajibu wake kama kiongozi wa nchi wanapaswa, kuogopwa kama ukoo. Kwa ninavyojua, rais Kikwete lazima awawajibishe ili kuwaonyesha Watanzania kuwa mambo yamebadilika. Atuonyeshe kuwa siasa za mazoea na kubabaisha zimeishapitwa na wakati na siyo stahiki na staili yake.
Kwa ufupi ushauri wetu kwa rais ni huu. 
Rais usiwavumilie nyani utavuna mabua. unayekaribia kumaliza muda wako ni wewe na ni wewe huyo huyo uliyeapa kulinda katiba ya nchi na si hao wapambe ambao wengi wao huwa ni nuksi. Rais Kikwete tuondolee kadhia. 
Wawajibishe mawaziri mzigo kwenye baraza lako la mawaziri kama hawa walioshindwa kutimiza wajibu wao kwako na kwa Taifa. Usiwape nafasi wakushangae au kukutisha.

Chanzo: Dira ya Mtanzania Oktoba 2013.