The Chant of Savant

Saturday 24 August 2013

Mlevi aanzisha Madudu Prize (MP)

Baada ya kugundua kuwa watendaji wengi wa lisirikali wanafanya madudu, mlevi amebuni mbinu nyingine mpya ya kuwapa moyo katika ufanisi wao wa kufanya madudu.  Kwa haraka haraka, naona bongo langu linaniambia kuwa mawaziri kama  Dk Harris  Mwakiembe, Porofwesa Anna Kajuamlo Tiba Ijuka, J4 Kawa-dog, Hawa wana Ghasia, Mizengwe Pinder, Makorongo Mahanga, Bill Lukuvy, Marry Nyagu, Emmy Nchimbvi na hata mkuu Njaa Kaya wanaweza kuwa washindi wa kwanza kabisa kunyakua tuzo hii.
Atakayeteuliwa kupokea Tuzo ya Madudu au Madudu Prize atakuwa akizomewa mara elfu moja ili ajirekebishe. Sambamba naye, hata yule anayepaswa kumtimua anayeendelea kumkingia fua naye atazomewa mara elfu mbili. Hebu mzomeeni kidogo.
Kwa vile mtandao wa wale wanaopaswa kupiga kura haujakaa sawa, watajwa hapo juu wanataarifiwa rasmi kuwa wameingia kwenye orodha ya wale wanaogombea kinyang’anyiro cha Madudu Prize ambayo itatolewa kila wiki. Tofauti na tuzo nyingine zinazolenga kuwapumbaza walevi, Madudu Prize inalenga kuwaamsha wapambane na wanyamawatu wanaowanyonya damu zao kwa kuwapa huduma mbovu kama vile elimu, simu, maji, umeme na mengine mengi. Hebu fikiria, kwa mfano, jinai aliyotenda J4 Kawa-dog ya kufelisha vitegemezi vyetu lakini akaendelea kupeta kwa vile anatoka sehemu moja na Njaa Kaya. Hebu fikiri urongo wa Ana Tiba Ijuka kututangazia kuwa angebomoa ule mjengo wa Ugabacholini na akashindwa. Kama Ana angekuwa na udhu basi angeamua kuachia ngazi au kuuambia umma wa walevi ni kwanini amri yake ya kuangusha ule mjengo imegonga ukuta. Je ule mjengo au wenye kuumilki nao ni lisirikali ndani ya lisirikali? Tuambieni tujue tuache kuwaghasi kama yule jamaa wa Hawa wana Ghasia anavyofanya ghasia.
Hivi itakuwa kosa kumpa tuzo rafiki yangu Jan Makamba ambaye hivi karibuni alipayuka hadi watu wakaanza kusema anapaswa aende Mirembe kupima akili zake mbovu? Kijamaa hiki ambacho kilipata ulaji kutokana na ukoo wake kuwa wa walaji kilisema eti kwenye upingaji hakuna sura ya urais wala uwaziri. Du! Hichi kijamaa hakina adabu heshima wala tabia. yaani hata mimi haoni nina sura nzuri kama ya rais na sura kama ya watoto wa wateule ingawa si mtoto wa mteule kama yeye? Hiki kijamaa kilisomea nini kiasi cha kuishiwa kiasi hiki na kuahidiwa tuzo ya Madudu? Kijana shukuru ufisadi wa kimfumo ambapo vigogo wanarithisha ulaji kwa watoto wao kama alivyofanya baba yako. Je wale wasio na baba vibopa wakatawale nyuni?
Wengine ninaopanga kuwapa Madudu Prize ni waishiwa watokanao na upendeleo au msukule kama watani wao wanavyowaita. Nadhani sihitaji kusema mengi kutokana na ukweli kuwa mzee Sam Sixx amewashukia vilivyo just  a few weeks a ago though he repudiated his allegations. Huyu mzee wa viwango anawajua vizuri kwa vile alikuwa bosi wao na isitoshe mkewe ni mmoja wao. So waishiwa wa dezo na zigo kwa kodi za walevi kaeni mkao wa kuliwa. Mmezoea kula wenzenu kupitia kodi zao. Sasa zamu yenu kuliwa. Au siyo?
Nilitaka kuwasahau maswahiba zangu ndata. Nyie mnaboa sina mfano. Tazama mnavyoanza kuwapa wahalifu ujiko. Kwanini juzi mlikwenda kumkamata mhuni aitwaye shehe Pondwa kiasi cha kufanya aonekane shujaa wakati hana lolote?  No Al Qaeda in my kaya Mr Pondwa. Acha ndata wakuponde ingawa nao hawana maana. Kama ni ushehe nami ni shehe tena wa kutegemewa na si shehena la chuki na mafarakano. Hivi inakuwaje mtu anaongea uongo kufikia malengo yake? Hakuna kitu kiliniacha hoi kama jamaa kudai eti lisirikali liliingia mkataba uitwao Memorandum of Understanding. Hakuna kitu kama hiki kisheria. Tatizo ni kutojua kikameruni. MoU ni makubaliano ya awali ya kuingia mkataba ila si mkataba. Sijui hawa wanaosikiliza upuuzi nao kwanini hawataki hata kujiendeleza? Someni muache kujitia aibu bila sababu kabla sijawapa Madudu Prize.
 DPP wamjua? Ni Director of Public Provocation aliyesema eti atamshitaki daktari Ulimbokie eti kwa kujiruhusu kuteswa na ndata. Je mwamjua kwa jina? Aitwa Eliyeza Fenesi. Na kweli jamaa fenesi.  Maana anavyofikiri na kutenda kama fenesi. Nasikia naye eti ni daktari. Kweli udaktari siku hizi si mali kitu. Au ni ule wa kughushi kama wa akina Nchimbis and Mahangas and Nagus and Nchimbiz and Kamalas?  Natamani naye huyu mshenz ateswe na mola wake kwa kufuru zake.
 
Bila shaka itakuwa si haki kumnyima tuzo ya Madudu mzee wangu na swahiba yangu Joni Tenda aliyepokea tenda ya kuvitenda wapingaji. Bwana Tenda nenda mwanakwenda kwani ushatutenda inshallah Maulana atakutenda kwa kukulipa kadri ulivyotenda.
Mwingine ambaye amejizolea Madudu Tuzo ingawa alishakitoa zamani ni zee moja la hovyo liitwalo Pita Kisumu. Hili zee kwa kujikomba kwa mafisadi sina mfano. Hata hivyo sisemi mengi zaidi ya kuliramba Madudu Prize ambayo pia itatolewa kwa Idd Lion kwa kukwapua mshiko wa Uda. Hili zee ndilo lilimponza DPP Fenesi aliyekula nalo njama kulifutia kesi wakati lilikwapua. Shame on you all!
Je mwamjua anayepaswa kuongoza katika kunyakua Madudu Prize? Leo simtaji japo kila mtu amjua. Wiki hii amenusuriwa na kasheshe ya Kageme. Nilipanga apate tuzo.  Baada ya kumtolea uvivu yule jamaa anayejiona yeye ni bora kuliko wote kama walivyodanganywa na wakoloni, nimeamua nisimpe kwa vile ametenda inavyopaswa. Njaa Kaya popote ulipo furahi umenusurika. Hata hivyo, ndugu yako Kawa-dog atakuonjesha ‘utamu’ wa Madudu Prize.
Kwa vile tuzo ya Madudu inafuata misingi ya ukweli na uwazi na kujitenga na uonevu na ufichi, nitaongea na da Flo Wingia, bosi wetu, afanye mambo wasomaji waweze kuchagua nani awe akiipokea kila wiki.
Wale wanaotaka kupata Madudu Prize wafanye madudu wataipata kirahisi na hata ndege watawazomea kwa kupata Madudu Prize. Uzuri wa tuzo hii hakuna cha kuhonga wala nini bali unapigwa kitu kama kilivyo.
Hint: Nilitaka kujinyonga niliposikia eti uongoziii wa vyoo vikuu unampigia debe Jan Makamba agombee urais. Du!  Urais kumbe umegeuka urahisi hivi! Ashindwe na anyong’onyee. Huna udhu wa kuwa rais. Unadhani watachagua mtu kwa ukoo wake? Go figure my friend.
Salamu kwa wateja wangu wa zama zile za Nkwazi Music Centres na Nkwazi Tanzania Vehicle Delivery Ltd.
Chanzo: Nipashe Jumamosi Agosti 24, 2013

No comments: