The Chant of Savant

Saturday 20 July 2013

Walevi wamstukia El Dorado Desperado Luwasha


Baada ya ziara ya Rais Black Obamiza kuwabamiza `mkenge’ walevi kwa kuhalalisha ujambazi wa Richmonduli, alipofungua mradi wa Symbiosis bint Richmonduli bint Dowans bint EPA bint Luwasha, kikao cha walevi kilikaa maeneo ya Yombo Vituka na kuja na yafuatayo:
Mosi, kutaka Waziri Mkubwa wa zamani, El Dorado Luwasha azuiliwe kupiga kampeni kabla ya uchafuzi wa uchakachuaji haujaanza rasmi.
Wanashangaa kuona jamaa akitapakaza `fweza’ zake kila mahali kwa kisingizio cha kupenda maendeleo ya walevi, wakati yeye ni yule yule aliyewahujumu kwa kuleta kampuni la kijambazi la Richmonduli, iliyobadilisha jina na kujiita Do-ones na baadaye Simbiosis Danganyika.
Pili, walevi wanataka tume ya uchakachuaji na li-‘sirikali’ waeleze ni kwanini wanaendelea kumfumbia macho jamaa huyo, anayeendelea kwa kasi ya ajabu na mbio za kutaka kuingia Kukuu huku akijulikana wazi asivyofaa hata kuwa mjumbe wa nyumba kumi?
Je, lao ni moja? Basi watueleze tujue ili tuwape hard time before vending us to swindlers and hyenas. Naongea `kimakonde’ kuonyesha kuwa sikughushi.
Tatu, walevi wanataka kujua ni kwanini jamaa hakufikishwa kwa pilato, baada ya kukwapua `njuluku’ zao kupitia kwenye sekeseke na `dili’ la Richmonduli?
Je, jamaa huyo yuko juu ya sheria, au ni kwa vile washirika na maswahiba zake wako juu ya sheria?
Nne, walevi wanawataka wapingaji `kushikia bango’ hujuma hii wanayofanyiwa na jamaa huyu, tena mchana kweupe. Je wamepitiwa au wamechanganywa na `mibomu’ wanayopigwa kila uchao?
Wapingaji mkiendelea kunyamaza mjue mmeliwa na imekula kwenu. Jamaa atawanyang’anya tonge mdomoni na muishie kulalamika na kulia bila kusikilizwa na wafwadhili mnaodhani wanajali. Wangekuwa wanajali, Obamiza angeshiriki kubariki dhambi hii ya Ubungo?
Tano, walevi wanamtaka Luwasha ataje vyanzo vya na namna alivyochuma huu ukwasi wake, anaougawa kama njugu kwenye nyumba za ibada na vikundi mbali mbali kama vile matching guys, anaowahadaa kuwaonyesha kuwa `anawadeku’ wakati anataka kuwatumia ili `akishaukwaa’ awakaange.
Jamaa anachuma kutoka kwa `magabacholi’ na kuwahadaa matching guys. Kama anawapenda si afukuze waganganjaa na wakimbizi wa kiuchumi waliofurisha mitaa yenu kwa biashara zao kichaa?
Pia ielekeweke, hawa wanaojiita watumishi wa God wakapokea na `kupwakia’ fedha chafu, hawana tofauti na mbwa mwitu. Hakika, hawa si watumishi wa God bali watumishi wa Dog aitwaye ufisadi.
Walevi wanataka kujua kama analipa kodi na kama vyanzo hivi ni halali au haramu.
Sita, walevi wanahoji hii aina mpya ya mapenzi ya jamaa ya karibu na uchakachuaji wa mwaka 2015. Je, haya ni mapenzi kweli au ni yale mapenzi ya binadamu na kuku?
Kwa msingi huo, walevi wanataka ‘Takokuru’, ile tume ya kulea na kuvumilia rushwa ifutwe kutokana na kushindwa kumzuia huyu jamaa kuendelea na kile ambacho kwa `kimakonde’ huitwa mega corruption, tena kwa kaya nzima.
Saba, walevi walevi wanauliza kama `Wadanganyika’ wako tayari kutendewa kama kuku ambaye huibiwa mayai yake na kuhongwa vipande vyake baada ya kukaangwa au kuchemshwa. 

Pamoja na ulevi wetu, sisi ni wajanja. Tumestukia mkenge huu unaoandaliwa ili jamaa `aukwae’ Ukuu halafu atutoe kafara ili kujilipa `njuluku’ anazomwaga kwa sasa.
Nane, walevi wanatamka wazi wazi tena kwa herufi kubwa na kinywa kipana kuwa kinachoendelea ni jinai na si haki hasa kwa demokrasia ya kweli. Kwanini mtu aanze kampeni kabla ya wenzake na iwe haki?
Tisa, walevi wanaazimia kuandamana hadi Ikulu na kwenye ofisi za tume ya uchakachuaji uchaguzi walioendelea kukaa kimya kana kwamba anachofanya Luwasha ni halali.
 Kumi, walevi wanataka Luwasha afunguliwe mashtaka ya kuhujumu kaya. Maana, jinsi wanavyoteswa na kulanguliwa umeme na migao hawana hamu na jamaa huyu?
Je, kuna kikundi au taasisi vinavyomuandaa jamaa huyu ili ‘atubamize mkenge’ mwingine kama swahiba yake aliyetuahidi vinono, akaishia kutupa vichungu huku akitugeuza sisi vinono vya wachukuaji waitwao wawekaji?
Kumi na moja, walevi wanamshauri asipoteze muda kuwaletea `njuluku’ zake chafu. Ingawa hili nalo limetugawa. Wapo wanaosema kuwa nimwalike aje tumlie na kumnywea `njuluku’ zake halafu tumpige chini.
Pia wapo wanaosema kuwa asikanyage kwenye baa yetu. Maana atainajisi na kutuchafulia jina. Wao wanasema kuwa ni heri wakose `kanywaji’ wabaki na heshima yake kuliko kufakamia `kanywaji’ kanakotokana na `fweza’ zilizopatikana kifisadi.
Juzi katika kumjadili jamaa huyu, nusu tutuoane macho kati ya tunaopinga na wanaounga mkono jinai hii.
Kumi na mbili, walevi wanahoji kwanini jamaa huyu hakuonyesha ‘mapenzi’ yake alipokuwa kwenye Uwaziri Mkubwa hadi akakubali kuingiza kampuni la-‘kijambazi’ kuja `kutubamiza mkenge’ kama tulivyobamizwa na Obamiza juzi juzi, baada ya kufungua mradi wa umeme wa Richmonduli uliobadilishwa jina na kuitwa symbiosis.
Kweli hii ni symbiosis. Kwa wasiojua maana ya symbiosis ni kwamba ni ushirika wa viumbe wawili au watatu wasiofanana kama Obamiza na Luwasha. Kisayansi chimbuko la neno symbiosis ni kigiriki, likimaanisha kuishi pamoja katika ushirika wa mashaka.
Kwa mfano, chawa na binadamu wanaishi kwenye mfumo wa symbiosis sawa na ule wa Richmonduli na Tanesco au walevi. Hivyo, walevi wanapinga hii symbiosis ambayo kwa lugha ya `kimakonde’ inaitwa ectosymbiosis.
Kwa wale waliosoma biolojia na kufikia kuwa na shahada ya juu ya PhD, wanajua fika kuwa kinachoendelea baina ya mafisadi kama hawa na lisirikali ni ecto and endosymbiosis.
Hata jinsi wauza gongo, bwimbwi na bangi wanavoishi na `ndata’ ni symbiosis. Hayo tuyaache ni ya wasomi waliochanganyikiwa lakini hawakughushi.
Kumi na tatu, je, hiki kinachoitwa misaada ya Luwasha siyo rushwa sawa na takrima inayolenga kuwaingiza walevi `mkenge’ ili hapo baadaye waishie kulia na kusaga meno?
Kumi na nne, walevi pia walimtaka Jeifo Kawa-dog, aachie ngazi baada ya kuendelea kuchemsha kwenye nyanja ya ilmu. Du, hii bangi na gongo! Yaani mara hii nimeishachanganya madawa!
Namshukia Luwasha kumbe na pombe inamshukia Jeifo! Mzee wa Kaya, tuondolee huyu jamaa yako. Anaendelea kuua future za vitegemezi vya walevi wakati vyenu mkipeleka ughaibuni kupata elimu bora kwa `njuluku’ zetu.
Mlimsikia swahiba na mshirika wake katika Richmonduli akijirusha kimanga kwa kujidai eti anakemea wanasiasa wanaoeneza chuki, huku akikwepa kuongelea wanaosambaza rushwa? Usanii mtupu. Salama kwa walevi niliowafundisha pale Biafra, Kinondoni na kwingineko.
Wabillahi tawfiq.

Chanzo: Nipashe Jumamosi Julai 20, 2013.

No comments: