The Chant of Savant

Saturday 11 May 2013

Mimi ni gamba tena nene


ccm
 Chama nambari wani kilipokuja na sanaa za kujivua magamba niliogopa. Magamba yalipo kipiga mkwara kikanywea. Badala ya kuyashughulikia yalikishughulia na yakaendelea kufanya vitu vyake.  Nami naona heri nijigeuze gamba lau nifaidi wafaidicho magamba. Siku hizi kuwa gamba dili babkubwa. Unageuka gamba na kukomba ili uzidi kutuna. Katika ugamba wangu nitaanzisha biashara ya kusafirisha madawa ya kulevya, pembe za ndovu na nyara za taifa. Kwa vile nitakuwa na gamba nene, hata uwanja wa ndege hawatanikamata. Simpo. Kama nitaona wale dog wa polisi wanaanza kunisumbua, nitaongea na jamaa zangu wa zima fire waniingizie kago yangu. Watashindwa nini iwapo nitawapa dau kubwa?
Tuache utani, taarifa kuwa watu wa zima fire wanatumia migari yao kuvusha bidhaa za wizi pale mwalimu Mchonga International Airport zilinfungua akili. Nilizibuka na kugundua ni kwanini mibwimbwi inajaa kwenye kaya. Kumbe jamaa ndiyo wanakula dili! Badala ya kuzima moto wanahangaika na wizi siyo? Ipo siku wataungua motoni waangalie. Ila waliniboa niliposikia kuwa wanachana mizigo ya abiria tena waliotoka majuu na kuiba vijisimu na vipapakatishi vyao. Wajua vipakatishi ni nini? Laptop au kompyuta lapa. Hayo tuyaache. Leo siwafundishi Kiswahili.
Nataka niwe gamba tena lile la nguvu. Najua nikishaunyaka ugamba nitapata mshiko wa nguvu kiasi cha kuficha kiasi kule Jersey na Uswazi ya Uswizi kabla ya kugeuka mfadhili wa miradi mbali mbali ya kiroho na uroho kama magamba. Nitakuwa nikiabudiwa kama magamba mengine. Nitatisha kama ukoma achia mbali miwaya. Lazima niwe gamba nifaidi bwana. Unadhani kuwa gamba mchezo?
Kuanzia leo naitwa mlevi Nkwazi Gamba nene na la haja.  Raha ya kuwa gamba ni kwamba unageuka mtakatifu. Dhambi zako zote zinasafishwa na unakuwa mweupe kama theluji. Nani hapendi kuwa kama theluji? Niongeleapo gamba hapa simaanishi lile jeusi la kobe na kasa. Ni gamba jeupe la utakatifu liliojaa utakakitu. Gamba la kitu si la kinyama mwitu kama kobe. Gamba na neema na zali na si gamba la konokono au kakakuona. Gamba langu lina nguvu kuliko hata magamba ya vyuo au shahada ambazo nimejaza nyumbani kwangu. Lazima nivae gamba.
Ukiwa na gamba wenye gwanda na magwanda hawakutishi. Badala ya kukutia adabu wanaishia kukujadili huku wewe ukijinoma na maulaji yatokanayo na kuwa gamba. Gamba bwana. Ujanja kupata gamba na si vinginevyo. Raha ya kuwa gamba ni kwamba unalinda kokwa ambalo mara nyingi ndilo humuihifadhi mdudu. Unahifadhi kokwa na kokwa linakuhifadhi.  Mnahifadhiana. Maana ukibanduliwa ujue ndiyo mwisho wa kokwa. Na gamba haliwezi kuota bila kuwepo kokwa. Kokwa haiwezi kuishi bila gamba. Hivyo, tunatumiana na kutumiana hadi tunaishi. uzuri wa kuhifadhi na kuhifadhiwa na kokwa si kama ule wa malkia wa mchwa ambaye huwaruhusu walume wampe urodas halafu akawaua ili wasijishaue kuwa walishiriki kikombe na bi mkubwa. 
Uzuri wa kuvaa gamba au kuwa gamba ni kupata ulinzi toka kwa watukufu wenye magamba mazito. Mara hii mmesahau jinsi gamba lilivyomuokoa Eddie Ewassa na Andy Chenge baada ya wapingaji kuwashupalia? Risasi za wapingaji hazikuwapata kwa vile zisingepenya kwenye magamba yao mazito. Hakuna kitu hunifanya ninywe na kucheka kama sanaa za jamaa yangu Njaa Kaya. Wajua? Akiwa ameuchapa ulabu si alijisahau akapayuka kuwa lazima genge lao lijivue gamba asijue gamba la kwanza yeye! Baada ya magamba mengine kuinyaka yakapanga mikakati ya kumvua nguo ili kila mtu aone gamba lake lilivyo nene kama yao.
Akiwa amemtuma Mapepe Napepea Ninaye kuwashambulia magamba wenzake bila kujua na yake wanayajua, Njaa Kaya aliishia kuuchomoa na kunywea huku Mapepe naye akizodolewa kwa kimuhe muhe na unywanywa wake. Mapepe alinywea kadhalika akakosa hata la kuwaambiwa waandishi wa umbea. Aliona aibu kuongea utadhani alikuwa na kiseyeye. Magamba yaliendelea kundunda hadi kutishia hata ulaji wa mweyewe. Asingestuka na kuufyata angeishia kuvuliwa gamba lake na kuadhirika huku wao wakiendelea kupeta kutesa na kusepa.
Kimsingi, rafiki yangu Njaa Kaya huwa na kaugonjwa ambako kitaalamu huitwa Payukayosis mental marasmus. Huu ni ungonjwa hatari ambao ukimpata mtu huadhirika mchana kweupe. Nakumbuka ugonjwa huu uligunduliwa mara ya kwanza nchini toka kwa mgonjwa aliyeitwa Yusifu Makambae Ngosi. Huyu bwana alikuwa ana kaugonjwa haka. Alikuwa akipayuka huku kinywa na ubongo vikikosa mawasiliano. Hata Mapepe Musa Nnaye naye ana kaugonjwa haka ingawa hakajafikia kiwango cha wagonjwa wawili wa kwanza.
Gamba ni kinga kuliko hata tunguli. Ukiwa na gamba hata ndata hawakuoni na wakikuona wanapumbaa wakikuacha ukifanya vitu vyako. Kama si gamba rafiki yangu Andaraman Kinamna angekuwa akikunyea mtondoo lupango. Baada ya zali lake la kusafirisha vipusa Mbali ya Mashariki kufichuka, ndata walitaka wamtie mikononi. Walipogundua kuwa kumbe naye gamba wakanywea. Kuwazodoa zaidi Njaa Kaya alimpa ulaji kwenye genge na kutuacha wengine vinywa wazi. Jamaa anazidi kutanua hata kwenda kutembelea miradi yake huko alikouza nyara za umma. Wajua? Nyara za umma hata ukiziteka nyara hakuna wa kukuuma maana huwa nyara za umma, sawa na mali ya umma, haziumi. Unaziuma na hakuna chombo cha dolari cha kukuuma angalau ukakoma.
Kayani kwetu lazima uwe gamba ndiyo uishi vinginevyo utajiishia sawa na walalanjaa. Nani alijua kuwa Roast Tamu La Aziz angeweza kufanya yote aliyofanya kuanzia Kagodamn, Downs, Richmonduli na uchafu mwingine na akaendelea kuula bila kuliwa? Gamba bwana! Ukiwa na gamba una kinga ya uhakika. Ndiyo maana nami napanga kuwa gamba ili wenye magwanda wakinilenga wanoe kama walivyonoa kwa magamba tajwa hapo juu. Nataka niwe gamba nono na zito kama mzee wa Kiwila anko Njomba Ben Nkapa wa Bill.
Chanzo: Nipashe Jumapili Mei 11, 2013.

No comments: