The Chant of Savant

Friday 24 August 2012

Somo toka maisha ya marehemu mzee Matonya

Picture
Ingawa marehemu mzee Matonya aliingia kwenye vitabu vya historia ya Tanzania kwa kile waingereza waitacho wrong reason, ameacha somo kubwa kwa wenye kufikiri. Taarifa zilizotufikia ni kwamba mzee huyu maarafu kama alama ya umaskini na ufisi wa taifa letu amefariki dunia. Mzee huyu mwenyeji wa Dodoma alikuwa kivutio kwa wengi jijini Dar Es Salaam ambapo yalikuwa makao makuu ya shuguli zake za kuomba. Kipindi fulani alimtoa jasho mkuu wa mkoa wa Dar Es Salaam wa wakati ule Yusuf Makamba alipomuamuru ahame na kuachana na shughuli za kuomba kwa sababu alikuwa akilidhalilisha taifa. Matonya hakukubali kufa kibudu. Alipambana na Makamba hadi kumtishia kuwa angemng'oa kwenye nafasi yake.

Sababu kubwa aliyotoa Matonya ni kwamba akina Makamba walikuwa walafi wanaokula kwa mikono na miguu huku wengi wakiangamia. Hivyo, kuomba kwa Matonya ilikuwa ni haki yake. Na kweli, kuomba ni bora kuliko kuiba au kujihusisha na ufisadi, mihadarati na jinai nyingine ambazo zimelifikisha taifa letu lilipo. Kwetu sisi Matonya alikuwa matunda ya siasa za kifisi na ubabaishaji. Pia Matonya alikuwa alama na kumbukumbu kwa wenye akili kuwa mambo hayakuwa sawa. Ni bahati mbaya kuwa watawala wetu hawakujifunza suto lililotokana na shughuli za Matonya. Badala yake walitaka kutumia maguvu kumficha ili asiwaudhi wao na wageni wao hasa wafadhili. Hakika huu mchezo umekuwa ukiendelea hata nje ya nchi ambapo wazungu huja Tanzania na kupiga picha za watu maskini na kuzipeleka kwao kutegeneza mabiloni kwa kisingizio cha kuhamasisha watu wao matajiri kuwachangia waswahili wenye dhiki. World Vision linaongoza kwa jinai hii. Inashangaza ni kwanini mamlaka zetu haziwazuii hawa wafanya biashara ya nafsi za watu kupiga hizo picha.

Tukirejea kwa Matonya, alikuwa shujaa aliyewabana watawala wetu. Hata walipowaficha maskini wengi vijijini, yeye alikharifu hujuma hii na kujitokeza na kuomba hasa jijini Dar Es Salaam ambapo ni moyo wa nchi. Matonya atakumbukwa Dar Es Salaam, Dodoma na Morogoro (alikoweka makao yake ya muda baada ya kutimuliwa kwa muda mfupi na Makamba kabla hajamdharau na kumshinda na kurejea Dar.)

Kifo cha Matonya ni pigo kwa taifa hasa maskini aliowawakilisha kwenye uso wa nchi kwa kung'ang'ania kuomba badala ya kuiba. Inashangaza watawala wanaosifika kwa kuombaomba kumfukuza ombaomba mwenzao. Je ni kwa sababu hakuwa ombaomba mwenye suti au anayetumia kalamu?
Nenda kapumzike mzee Matonya ulikuwa changamoto kwa wenye akili na udhu.

3 comments:

Anonymous said...

wewe na matonya hakuna tafauti ila yeye kava shuka wewe matonya wa ulaya

Anonymous said...

Anon 07:11 huwezi kuelewa kilichomaanishwa hapa. Kwa watu wenye mawazo mafupi kama yako Matonya hakuwa chochote. Umechangia matope na ushindwe na kulegea.

Yasinta Ngonyani said...

Astarehe kwa amani!