The Chant of Savant

Wednesday 11 July 2012

Nani anapenda wabunge wanaowashwawashwa?


HAYO si maneno yangu bali mwenyekiti wa mjengo bwana mkubwa saana tena saana, Steve Mambumba wa Mambumbu alipomtolea uvivu dogo Joni Mnyika kuwa anawashwawashwa.
Alikuwa akiwashwawashwa wapi? God forbid nisitukane waheshimiwa wasio na heshima bali uhuni mtupu ingawa si wote.
Ukiondoa jamaa zangu wa upingaji, wale wa Chama Twawala kweli wanawashwawashwa kama alivyosema mwenyekiti wao bingwa wa kuwashwawashwa hadi akatumia lugha ya kihuni utadhani yuko standi ya mabasi Mwenge.
Tukubaliane kuwa kama wabunge wetu ni hivi basi kaya ina kibarua kikubwa tu.
Kabla vumbi la kuwashwawashwa halijatua si mwingine mwenye kuwashwawashwa aitwaye Musa Machale alitolewa nje na mzee wa kuwashwawashwa eti kwa vile ana alichokiita kiherehere cha kudandia mambo yasiyomhusu utadhani mambo ya mjengoni haya kuwa yakimhusu.
Sisi kijiweni tuna nidhamu ya ajabu. Hakuna anayeruhusiwa kumfanyia uhuni mjumbe au kumpachika sifa za kihuni kama alizowapachika wenzake huyu Steve Mambumbu.
Maana tunaamini kijiweni kuwa kila mwakilishi ajaye pale anawakilisha walevi. Hivyo, ukisema mwanakijiwe anawashwawashwa maana ni kwamba walevi wote wanawashwa washwa.
Je, ni kwanini walevi na wagonjwa hawa wanapenda kutukana watu tena wanaowalisha? What a heck of goons so to speak! Samahani maana mzuka wangu ukipanda namwaga ng'eng'e ila mbaya.
Mwingine aliyeonyesha kuwawashwawashwa ni dada yetu aitwaye Stella Matomatoes. Huyu alikuja na mpya kwa kuwashwawashwa na kudai kuwa Chakudema ndio waliomteka Dk. Steve Walimboka na kumfanyia uhuni wakati ukweli ni kwamba waliomteka si Chakudema bali Uhasama wa Taifa walioagizwa na mabwana zao wanaowafuga.
Wengi wa wajumbe walihoji utimamu wa dada huyu anayeonekana msomi kumbe bomu! Kumbe kuwashwawashwa ni ugonjwa mbaya sana unaoweza kumfanya mtu afanye mambo ya ajabu kama da Stella pamoja na ubukuzi wake wa mainjini hadi akaitwa injinia.
Nani aliamini kuwa da Stella angewashwawashwa hadi akaongea uongo na upuuzi? Hayo ndiyo matokeo ya ugonjwa wa kuwashwa washwa.
Inawezekana da Stella anasumbuliwa na ugonjwa mwingine wa kiherehere. Kitaalamu kuwashwawashwa au Itchiosis washwawashwing ni ugonjwa unaoweza kusababishwa na mambo makuu mawili.
Mosi, madhara katika ngozi (Dematoscratchiosis) au madhara katika ubongo (Cerebitchiosis). Wahusika hapo juu wanakumbwa na category B yaani Cerebitchiosis.
Siku bingwa wa kuwashwawashwa, Steve Mambumba alipowashwawashwa akisaidiwa na da Stella, hakuwa peke yake. Ukiondoa Machale na da Stella, mwingine aliyewashwawashwa ni jamaa yangu kijogoo Mwijuu Mchembe aka Nchemba.
Huyu bila hata chembe ya kutumia ubongo aliunga mkono miwasho na upupu wa da Stella kiasi cha wenye akili kudai kuwa huenda kwa vile yeye ni kijogoo alikuwa akifanya hivyo ili kupiga chapuo maana fisi huwa hachagui mifupa. Whether Sister Matomato is kidosho, mkangafu or kizee hayo hayanihusu.
Utafiti unaonyesha kuwa wagonjwa wa kuwashwawashwa huwa hawafikirii vizuri. Hii ndiyo maana badala ya kuwalaani wale mbwa waliowashwawashwa wakatumiwa na wenzao kumteka na kumtesa daktari mwenzetu Walimboka, walikimbilia kuwabambikia kesi wenzao.
Mie naona akina Matomatoes na Mchembachembu walipaswa kuwa mandata mabingwa wa kubambikia watu kesi.hawa jamaa zangu kina da Stella na Mwijuu wasingekuwa na ugonjwa wa kuwashwawashwa wangejua kuwa dingi wao Njaa Kaya ana ugonjwa wa kuwashwawashwa kiasi cha kujipayukia akidhani mgomo wa matabibu ni jambo la kawaida sawa na kwenda Brazil kusogoa na kina Maximo.
Angejua akina Zein bin Zini ben Ali waliondolewa kwenye ulaji kwa tukio la kijana mmoja aitwaye Mohammed Boazizi kujinyotoa roho kwa kujiwasha, asingecheza makindamakinda kama mama microfoni Anae Makida Makida.
Hata hivyo tusiwalaumu sana kina da Matomato na Mwijuu. Ulaji wakati mwingine waweza kusababisha ugonjwa wa kuwashwawashwa. Nani mara hii kasahau rafiki yetu Tunituni Ben wa Makapu alipolewa ulaji akawashwawashwa na kuwaita walevi wenye uvivu wa kufikiri na wivu wa kike utadhani...
Muulize leo kuhusu tambo zake. Hana bao zaidi ya kuishi chini ya hisani uchwara ya mkuu wa kaya hii.
Pamoja na ubobezi wangu kwenye udaku na udakuzi, sikuwa najua kuwa kumbe Mwijuu Mchembe alikwapua fweza kwenye soo la HEPA lililompa tafu jamaa yangu kuwahonga walevi na kumpa kura ya kula jamaa yangu ambaye leo nisingependa nimtaje kwa vile yeye HEPA ni mapacha.
Yote katika yote najiuliza swali moja: Hivi kwa kuwa na wawakilishi wanaougua ugonjwa wa kuwashwawashwa zaidi ya kuiwasha nchi kwa moto wanaweza kuleta maendeleo gani?
Nani anategemea maendeleo hata mawazo ya kimaendeleo toka kwenye mjengo uliogeuka uwanja wa mipasho ya kina Adija Kopo?
Jamani mzee mzima sizushi. Nenda pale mjengoni uone watu wanavyowashwawashwa hadi kushindana kubofya Blakiberi badala ya kushiriki mijadala. Huu mjengo naapa si mjengo kitu bali mjanga.
Kuanzia sasa napendekeza mjengo uitwe mjanga maana unatengeneza janga kwa taifa kama unaweza kushindwa kulaani kitendo cha kupigwa dokta Walimboka na badala yake wagonjwa wa kuwashwa washwa wakaanza kuisingizia Chakudema.
Mie nawalaumu Chakudema kwa kuendekeza ustaarabu na kukaa kimya badala ya kuwapa wazi kuwa waliomteka Dokta Walimboka na Uhasama wa Taifa wanaotumiwa na Chama Cha Matesaji (CCM), sio CCM hii, kutaka kuwatisha na kuwanyamazisha matabibu.
Kwani huu uongo? Wambie wakanushe tuwape data zote. Kuhusu ujambazi wa HEPA kama siyo Mwinigulu Mchembe kuokolewa na da Jeni-star Mhaganama, huenda nyeti zake zingekuwa mitaani kama ilivyokuwa wakati ule alipofumanika kule Igunguli alipokuwa akivunja amri ya Mungu na mke wa kada mwenzake wakayamaliza kimya kimya kama rafiki yake Lionichawene.
Mi siku zote naomba miwaya na umeme uwakongoli hawa jamaa wanakwenda kwenye mjengojanga kutangaza ujogoo wao kama jamaa yangu pale kitaa cha Magogoni.
Kijiwe kikiwa kinajiandaa kutoa karipio kwa hawa wahuni wenye heshima si tukasikia kuwa ugonjwa wa kuwashwawashwa umewakumba hata Takokuru kuja na kiherehere kuwa watafuatilia mabilioni ya mshiko yaliyofichwa na majambazi wakubwa kule Uswisi.
Mara ghafla umeme ulikatika kila mtu akachukua hamsini zake! Unacheza na maisha bora ya kiza kwa wote siyo?
Chanzo: Tanzania Daima  Julai 11, 2012.

No comments: