The Chant of Savant

Wednesday 27 June 2012

Kumbe wadhauliwa machizi!



Joni Mnyika ametufungu macho ingawa tulikuwa tukijua. Tuliogopa kuonekana wachochezi. Sasa wanaitana machizi wenyewe sisi tuwaite nani?
kutokana na mzee mzima kutoongea kwenye kikao kwa muda mrefu, leo nimelianzisha kwa kutaka kujua mawazo ya wana kijiwe kuhusiana na akili za waheshimiwa wao mjengoni.
Swali langu lilianza hivi: Jamani, hivi hawa waheshimiwa wa chama kilichopo kwenye ulaji ni wazima kiakili?
“Dk Mgosi Machungi anakuwa wa kwanza kula mic, “Kama titawaangaia kisaikoojia, hawa jamaa ni machizi kama aivyosema Joni Mnyika. Maana timeshuhudia wakipitisha vitu vya kipuuzi kuonyesha wasi wasima kiakii. Isitoshe kama wao wanaitana machizi unataka sisi tiwaiteje zaidi ya machizi fyatu?”
“Du Dk Mgosi unachambua kama vile wewe ni daktari wa saikolojia!” Alichomekea Dk Mbwa Mwitu.
Dk Mgosi kasifiwa anaamua kurejea, anasema, “Kwani saikoojia umeona ni somo kubwa kuiko yote? Kwa taifa yako timesoma haya mambo tena kue kue ushoto kama hujui ujue.”
Kijiwe hakina mbavu kwa jinsi anavyosifia Lushoto utadhani Oxford.
Tukiwa tunacheka, Dk Mipawa amepata upenyo kutongoa, “Huyu kijana Joni kwanza namfahamu sana. Alikuwa mwananfunzi wangu na isitoshe baba yake huwa tunakunywa wote bia sometimes niwapo na pesa. Alichosema kijana ni kweli hasa ikizingatiwa kuwa waheshimiwa wetu wengi hasa wa chama twawala wanawakilisha matumbo na si majimbo yao.”
Kabla ya kuendelea Dk Kidevu anaingilia, “Hakuna mheshimiwa mdharauliwa na mpuuzi kama wangu. si mlisikia alivyokumbwa na kashfa ya kusafiri na zana za kivita utadhani alikuwa Somalia? Kama siyo mkwerere kumuokoa, angekuwa analia kama bosi wange Bill Ngereza.”
Dk Maneno anachomekea haraka, “Unasema hicho kitoto kilichodandia kwenye umaarufu wa baba yake?”
“Ndiyo. Siku hizi umekuwa ndiyo mtindo wa maisha. Riz kwenye mgongo wa Njaa, Sal kadhalika naye, kwanini hichi kizinzi kisitumie umaarufu wa dingi wake?”
Dk Mpemba anachomekea, “Mie naona huyu kijana hata kama wa hovyo mwamuonea. Mbona wako wengi njengoni walioingia kwa umaarufu wa baba zao? Wategemea nini toka kwa watu waloingia njengoni kwa kutegemea umaarufu wa baba au mama zao, kuhonga, kughushi na kuchakachua?”
 
Profesa Dk Msomi Mkatatamaa anaamua kula mic naye, “Ule mjengo ni wa machizi hasa ukiondoa waheshimiwa wa upingaji na wachache wasio watumwa wa ufisi. Hivi unategemea nini toka kwa watu kama LivingJiwe Lushindo, Annae Abudala, Sofia Lion hata huyo bosi wao ambaye juzi alinichekesha kudai eti waache matusi na kurejesha heshima ya mjengo wakati yeye ndiye chanzo kikuu cha aibu na uchizi wao?”
Kabla ya kuendelea, Dk Mchunguliaji anachomekea, “Hamkumsikia Joni Ngereza akitapika mbele ya wenzake kwa hasira ya kunyang’anywa ulaji? Mie naona tungeondoa mjengo ili watu wachache waache kututumia. Maana zaidi ya kuwawakilisha wake zao, watoto zao na matumbo yao hawatuwakilishi zaidi ya kwenda kule kutuchuuza.”
“Kama kuna chizi si mwingine bali kile kijimama shangingi na changu kinachosimamia hawa machizi. wajua nimaanishacho. Annae achezaye Makindamakida.” Aliingilia kati Dk Mipawa.
“Mie naona hata mkuu angetimuliwa maana naye ni chanzo cha upuuzi wote huu. hivi wadanganyika hawaoni anavyowalostisha kwa matanuzi na kuruhus mamisab wake na kitegemezi ukiachia mbali waramba viatu kuiba njuluku zetu?” Alichomekea Dk Kidevu.
Dk Mpemba hakujivunga; alikamata mic, “Mie naona heri tuwe hatuna lisirikali tokana na kutuumiza sana. maana watufanyia vitu vya ajabu ajabu.”
Kabla ya kuendelea Dk Machungi alidandia mic, “Ami mbona hatikueewi. wanamifanyie vitu vya ajabu ajabu vipi au popo bawa?”
Dk Mpemba, “Mambo ya popobawa waulize kina Lushindo na mkuu mwenyewe na Simbacheni waniojua kuchovya huku na kule. Mie simaanisha mambo ya Popobawa yakhe. Naamisha huu wizi wa fedha zetu. Ingawa twasema wao machizi nasi machizi maana twaibiwa nchana.”
Kabla ya kuendelea Dk Mipawa anadakia, “Nkwingwa, kwanza lushindo kikwetu matusi makubwa tu. Je ni kweli Simbacheni amefumaniwa na mke wa askari au siasa za mitandao?”
Dk Profesa Mkatatamaa baada ya kuona mambo ya popobawa na mafumanizi ya Kimchembachemba yanaanza kutawala anaamua kuvaa daruga kurejesha mada kwenye mstari. Anasema, “Mie mambo ya kufumaniana hayanihangaishi kama uchizi wa hawa jamaa ambao wanapitisha libajeti linaloumiza wale wanaowawakilisha.”
Kabla ya kuendelea, Dk Machungi anaingilia, “Mgosi, usiseme eti wanawakiiisha watu. hawatiwakiishi bali matumbo yao. hivi ni mdhaauiwa gani anawakiisha yeyote zaidi ya mabwana zao, chama chao na matumbo yao.”
“Unamaanisha hata makamanda wa magwanda wa upingaji nao nyanya?” Aliuliza Dk Mbwa Mwitu.
“Hapa hatuongelei jamaa wa upingaji kama vile Mzito Kabwela, Mtuhuru Mboe, mchungaji Msigua, Hole Lissu, Joni Mnyikani na wengine machachari. Hawa si machizi ni machizani.” Alichomekea Dk Mchunguliaji.
Nami profesa mzima kuona chansi nikaamua kuitumia na kusema: Mie naona wote machizi sema uchizi wao unatofautiana. Wale wa Chama Cha Mafisi fisadi (CCM) ni machizi wa kughushi, kujuana, kulindana, EPA, Richmond, usanii, ujambazi na madhambi yote wakati wa upinzani ni machizi wa Ukombozi.”
“Du! Kweli wewe profesa kuliko hata yule profesa wa Kafu wa pumba. Nimekukubali kichaa wangu. Yaani kwa mtindo huu unaweza kusema na mkuu ni chizi wa usanii na dogodogoz au siyo?” Alidakia Dk Mchunguliaji.
Dk Profesa Msomi anakatua mic na kuendelea, “Kwa taarifa yenu kaya hii kila mmoja ni chizi ndiyo maana kila mtu ana nafasi ya kufanya uchizi.”
Kabla ya kuendelea Dk Machungi anaingilia, “Ami una maanisha hata sisi ni machizi tinaofanya mambo ya kichizi au una mpango wa kutitukana siyo?”
Dk Profesa Msomi anakatua mic tena huku akimalizia kubwia kahawa, “Sasa kumbe. Bila kuwa machizi tungeruhusu vipi machizi walipane mishiko kuanzia ya matako sorry makalio hadi umbea bila kuingilia kati?”
Dk Mgosi, “Kwani sisi tinakwenda kwenye mjengo?”
Dk Profesa Mfilosofe Msomi, “Tunakwenda mjengoni kwa kukubali kuwakilishwa na machizi kama alivyosema dogo Joni Mnyika. Hakika huyu dogo jina Lake Limanfaa. Maana ni nabii aliye nyikani. Bila kuwa machizi tungekuwa tumeishaingia tahrir kuondoa uoza huu. You know what I mean.”
Tukiwa tunaendelea kutongoa si daladala moja likaturushia maji machafu kiasi cha kwenda kumtia adabu dereva wake!

No comments: