The Chant of Savant

Sunday 21 November 2010

Bai bai Samm Sixx ndiyo uchakachuaji huu ati

Niliposema kuwa mimi ni mtafiti na mvumbuzi wengi walinicheka na kunikejeli bila kujua.

Maskini hawakujua. Hawakujua kuwa nimevumbua mbinu mpya ya kuwa mkuu wa kijiwe! Kabla sijazama kwenye thesis yangu lazima niseme: ukitaka kuwa mkuu lazima ujenge ufalme wa familia. Bila hii, ukuu utausikia kama Dokta Silaha au Sammy Sixx na usipika.

Baada ya kuona walionizunguka kijiweni ni wasaka ngawira na vyangu wanaoweza kumtumikia yoyote kama toilet tissue niliamua kuunda ufalme wa familia ili kuukwaa ukuu wa kijiwe.

Japo nilimtumia mgosi Machungi wa Makambale na mwanae, hawakunishawishi kutokana na tabia ya mgosi kupayuka hovyo. Hata hivyo tusimlaumu sana. Shule, shule bwana. Hamkuona akina Tambo Hizo walivyochemsha wakitaka kunifurahisha kwa kuwaongopea walevi?

Baada ya kugundua udhaifu wa kambi yangu, nilijipanga upya na kuja na mpya.

Hatua ya kwanza ya kufikia ufalme huu japo uchwara na wa muda ilikuwa ni kuwamotisha bi mkubwa na kitegemezi changu.

Hatua ya pili ilikuwa ni kuwaamrisha vijana wangu wa usalama kuhakikisha nakuwa mkuu tena.

Bila wao zengwe la Zenj lingeninyotoa roho. Maana kama si wao kunishauri nimbebe huyu daktari Blaah Blaali huenda pangechimbika bila jembe. Pia walifanya jambo la maana kunishauri kumtosa wa Kusheini ili asijeharibu dili hapo 2015 kwa kuwa maarufu zaidi ya mshikaji ninayemuandaa kunilinda baada ya kuachia ngazi.

Ilibidi nijipange kweli kweli mimi na nyumba yangu ili kunusuru ulaji na madili yetu ukiachia mbali kuhofia kuja mtu mwingine akatutupa lupango.

Hapa ndipo nilipogundua sayansi ya karne hii ya kuukwaa yaani kuchakachua. Hata hivyo, inabidi niwashukuru waliovumbua uchakachuaji orijino. Nichukue fursa hii kuwashukuru wachakachuaji wa wese walioniwezesha ku-modify kanuni ya uchakachuaji na kuweza kuchakachua kula za kura.

Na bila hii nisingeshinda kuongoza sorry kuibia kijiwe kwa kishindo cha uchakachuaji. Kishindo cha uchakachuaji kilikuwa kikubwa kuliko hata Tsunami. Na niliposema nitashinda kwa kishindo nilimaanisha uchakachuaji.

Sasa wale maadui zangu wakuu wakae mkao wa kuliwa. Hamkuona nilivyomwaga manonihino Sammy Sixx aliyetaka kuangusha ulaji wangu siku za nyuma hadi akasababisha swahiba zangu kama Eddie Ewassa kutimliwa kama kibaka hata kama alikuwa kibaka?

Walipomshauri ahame chata yetu na kujiunga na wapingaji wetu alidharau asijue nilikuwa namlia timing. Maskini Sixx. Hakusoma alama za nyakati na kujua jinsi mambo ya mitandao yanavyokwenda. Hata hivyo, ashukuru Mungu. Bila shinikizo la walevi tungemwengua mapema na akawa anausikia mjengo magazetini kama Selelii na wale wote tuliowaengua kutokana na kufuatilia ulaji wetu.

Hapa inabidi nitoe onyo mapema. Yeyote atakayejifanya kuingilia ulaji wetu ajue atapata cha mtema kuni. Maana kipindi hiki nitakuwa bonge ya dikteta bila kujali lolote. Maana baada ya lala salama hii sina mpango wa kuwania ulaji zaidi ya kutafuta kibaraka wa kunirithi na kunilinda mimi na Tuni Tuni.

Tuendelee na masahibu ya Sixx. Kwa wajuzi wa kiarabu watanielewa. Ukitaka kumla panya huwezi kumuita panya. Unamwita Hamaam al wadi au hua wa wandani. Hata nasi tulipotaka kummaliza jamaa ili asitorokee kwenye ukinzani tulimtisha na hatimaye kumpitisha ili ajidanganye kuwa tu kwenye safari moja. Pia tulimsifu asijue alikuwa anameza chambo! Sasa atakaa benchi na akija na michango yake ya kutaka kuharibu ulaji mtu wetu kwenye kiti kikuu anampiga stop.

Kwanini kukaa na mtu anayepata umaarufu kuliko hata mimi? Sumu yangu ni mtu kujulikana kuliko mimi. Nikiona unaanza kujenga umaarufu na kukubalika lazima nikusukie zengwe uishie bwana. Hata bi mkubwa akijitia kujua kujua na biashara zake na kukaribia kunizidi umaarufu namwacha na kuoa mwingine. Na ngwe hii sitamruhusu kunifuatafuata kila niendako ughaibuni kutanua. Kwanini awe na mtima nyongo wakati ulaji wake nimempa wa kutosha? Nami aniachie nitanue na dogo dogos bwana. Maana maisha ni nipe nikupe.

Kijiwe kimechoka na aibu ya kufichuliwa maulaji yake tena hili likiwezeshwa na mtu aliyedhaminiwa na chata letu la Uchakachuaji. Kwanini mtu anayevunja sera yetu ya kulindana na kujuana asipatilizwe badala ya kuwapatiliza mashujaa kama Ewassa na Chenga? We can't let our kijiwe go to dogs even if we are dogs. But we are big dogs not skinny ones. Samahani nikipandisha mwenembago huwa kiingilishi kinapanda pia.

Pia nichukue fursa hii kuwaonya wapingaji. Nasema. Mtajijeijei mna dola nyie?

Sasa baada ya kuushikilia mjengo wale wapinzani wangu ndiyo wajue nimewamaliza. Maana walipata umaarufu wao kiasi cha kutaka kunitimua kukuu kutokana kupewa nafasi na Sixx. Sasa hamtawasikia tena na lazima uchakachuaji ujao chata langu lazima lipete kama kawa.

Baada ya kuchakachua kula na sasa nafasi ya microphone, ngoja muona washirika wangu ama watoto zao watakavyojaa kwenye baraza langu la wezi sorry mawaziri. Washikaji wangu wawe wa kike au wa kiume lazima wapete na kupetuka wakati nyie mkiteseka. Hata hivyo msikonde. Nshasema: raha jipe mwenyewe usingoje kupewa.

Na kwa wale waliotaka kuingilia mbio zangu za kurejea kwenye ulaji wajue sitawasamehe. Wasidanganywe na bashasha zangu. Mie ni katili kuliko mnavyoniona au kunidhania. Anayebisha akawauliza akina Babu Seya na hata Sixx.

Msichachawe na kuchanganyikiwa bure. Bado sijamaliza majadiliano na bi mkubwa na kitegemezi changu kuamua nani aingie na nani atemwe.

Utemaji wa Sixx haukufanywa na bunge langu kuu yaani bi mkubwa na kitegemezi changu. Huu ulifanywa na kina Ewassa, Roast Tamu, Endelea Chenga na Mgosi Machungi Makambale. Kawaida ya chama chetu ni kumruhusu anayemaliza muda kugombea tena. Lakini kwa kesi ya Sixx hatukuwa na jinsi. Ilibidi kuukiuka huu utaratibu wetu. Najua wengi watasema mimi ni mnafiki kwa vile niliwazuia waliotaka kugombea ulaji wakati mie ndiyo nilikuwa bado incumbent kama Sixx.

Hata hivyo mgosi Makambale asiwatie hofu. Licha ya kudhoofu kiakili na kiafya, nshamchoka kutokana na kuniletea matatizo kutokana na kupayuka kwake kusiko na mantiki wala maana. Kwanza amenitisha. Mie nimesotea ulaji na ukuu. Hivyo, ninastahili kuwaingiza kwenye ulaji wangu bi mkubwa na kitegemezi changu. Bila kutoa jasho lolote eti naye analeta kitegemezi chake kuunda ufalme mwingine ndani ya ufalme wangu. Lazima muhura huu nimtimue ikiwezekana nichukue kifaa toka Somalia.

Hata hivyo, lazima nitafakari. Kifaa toka Somalia kina nongo nyingi hasa kugundulika kuwa kinajihusisha na utoroshaji nyara. Lakini hata hivyo nani anajali iwapo mimi ni yote katika yote na juu ya yote? Hapa ni kuwashawishi washirika wangu yaani bi mkubwa na kitegemezi wakikubali na wasikwaruzane nacho kutokana nao kuwa na dili zao. Hivyo kwa mtu mwenye kusaka ngawira kama wao lazima kuwepo na mgangano nisipokuwa makini.

Naona shangingi la Mr Sixx likipita! Acha nimmpe pole kwa kulipiziwa kisasi Njaa Kaya bin Mchakachuaji.
Chanzo: Tanzania Daima Nov. 17,2010.

No comments: