The Chant of Savant

Wednesday 2 April 2008

Kijiwe kiliposhuhudia maajabu matatu

Wiki hii kijiwe kimeshuhudia maajabu matatu. La kwanza ni kufanyika kwa mikutano ya kufuru dhidi ya misingi aliyoweka mzee Mchonga, kule Mwitongo ambapo kama kawaida CUF iliishia kutapeliwa. Pili, Mkuu kuanza kuwageuka makanjanja waliomsaidia kuangusha bonge la Tsunami kwa wabongo walipotwishwa bonge la mkenge. Mwisho, kuingizwa mjini kwa tapeli wa kiroho na watoto wadogo mchana kweupe na mbele ya runinga. Hapa hatujaongelea ule wa Comoro tukiiacha Zenji na kusuluhisha Kenya.

Tumeamua kukutana Mikocheni baada ya Kariakoo kujaa vinyesi vya mafuriko, mara zilikuja nyuzi kuwa maombo ya kiroho ya Dr. Ulaji Rwakatarehe yamesababisha misukule kuanguka kanisani!
Hao! Tulitimka kuona kulikoni.
Endelea na stori toka kwa washikaji wenyewe.

"Huyu mama daktari wa ulaji kama Komandoo feki ashazoea tapeli watu kuwa yu aombea watu. Mie nilinstukia alipopwakia ubunge uchwara wa ubuge wa Nambari wani. Yakhe umeona vichanga vilivomtoa nishai? Ama kweli mwezi huu umekuwa wa utapeli mtupu sawa na Nkuu alivyohadaa watu eti amuenzi Mchonga ilhali abomoa kila jema alilofanya!" Alilianzisha Mpemba.

Mara Mgosi Machungi anadandia akiwa na jazba sina mfano. "Tiishasema maa nyingi. Hawa wachungaji wanaochinja mifuko ya watu wa Mungu watakuja kuumbuka vibaya. Sasa ona daktai wa kupachikwa anavyohaziika jamani. Ingekuwa Ushoto huyu angepigwa zongo nasema."

Mkurupukaji hangoji. Anakurupukia mic. "Hawa wanadhani Mungu ni kama Chama lao na wadanganyika. Na bado watazidi kuumbuka tena kabla ya kufa hapa hapa duniani. Kama wanajua kuombea miujiza mbona hawakuzuia mafuriko wala wizi wa EPA na badala yake wameushiriki na hizi hadaa za Butiama? Hawa nao ni matapeli sawa na wenzao. Hawa nao ni mafisadi tena wa kiroho. Ni wa kuogopwa kama ukoma yakhe na Mgosi."

Mzee Maneno naye anakatua mic. "Mie ya Butiama hainistui. Maana Mchonga mwenyewe ndiye aliyetuachia Mjasiriamali asijue ni kibaka wa kawaida. Hili la huyu Daktari Ubwabwa bin Ulaji wa Mikocheni nalo linafurahisha. Hivi wana hizaya hawa wangekuwa wanaombea watu Kaya yetu ingegeuka jamvi la akina Jeetu Patel na Malegesi kujikombea? Naona tungewatolea uvivu hawa. tuwalambe bakora. Hongera watoto wadogo: kuwaumbua watu wazima wanaofanya mambo ya kitoto."

Leo Mchumia tumbo hayupo. Yupo Butiama kula makombo ya mafisadi.

Mbwa Mwitu anatia buti kwa mbwembe. Anakwanyua mic. "Mnashangaa hili la watoto kumuingiza mjini daktari Ujuha! Kwanini hamshangai la Mkuu kujitia mwalimu wa maadili ya uchonga peni! Eti leo anakaripia makanjanja wakati ndiyo hao hao waliotuingiza mkenge tukampa ulaji! Mbona anao tena kwenye ofisi yake! Au mmemsahu Nshomile wa Richmond anayefanya uchafu wake pale Ikulu? Kama yuko serious mbona hamtimui wala kutoa sababu za kumteua kwenye sehemu nyeti kama hiyo?"

Anakamua kombe lake na kuibusu kashata na kuendelea kumwaga cheche. Sijui leo aliamkia baa gani? Maana anavyopokoma utadhani naye ni Daktari!


Anatongoa. "Mie naona Kaya hii imegeuzwa uwanja wa matapeli. Hukusikia yule Ole Naikose alivyokuja na mpya kuwa Ewassa Mmeru alitimuliwa ili kuwapuga akina Ole?
Mungu huyu! Unajua ameishaumbuka baada ya kuunganishwa kwenye kashfa ya TICTS? Na bado. Mama wa utapeli ni EPA ambapo waliohomoa eti ndiyo wanaowakamata waliohomoa nao! Wajameni. Nahisi aibu kuitwa Mbongo sasa."

Makengeza naye hajivungi. Anamwaga radhi. "Tukubaliane. Kaya hii imewashinda kiasi cha kujipeleka Butiama ili wavuane nguo. Umelisikia zengwe la Mr. Six na viwango vyake vya kula njuluku milioni mbili kwa wiki kwa kununua madawa? Sijua anaumwa gonjwa gani aghali hivi?"


Mara mzee Ndomo naye anaamua kutoa zake. "Huyu mama aliniacha hoi alipokuwa akijinadi kuwa anawajaza watu ukwasi ilhali anausaka kwenye nambari wani tena wa EPA! Hakuna siku aliniua kama alivyodai anaombea ndoa wakati yeye hana! Hujamsikia tapeli wa kiroho aliyebanwa akasema atashitaki mahakamani badala ya kwa Mungu?"

Mara Mgosi anachomekea. "Tinamjua ni Katortoise huyu. Hata huyu Gamanyuwa naye ni tapei. Pia nimewasikia wa kule Zenji waliompa kibuti Owassa aipomwagwa nonihino. Ni vituko kwei kwei Kaya hii!"

Naona Msomi Mkata tamaa hataki apitwe. Anatia guu baada ya kupiga busu kwenye tangawizi lake. "Nyinyi kumbe mlikuwa hamjui kuwa Kaya inapokaribia kusambaratika, kila mtu hutumia kila mwanya kuiibia! Hawa watu wa Bwana ni washirika wa mafisadi. Wanawaibia kwa kuwakaribisha kwenye harambee za kuchangia maduka yao yaitwayo makanisa. Hawa ni sawa na fisi mbele ya simba. Kila alipo simba fisi wapo kula mabaki. Huyo mama angekuwa mtu wa Bwana asingeingia kwenye ubuge wa nambari wani iliyokosa mwelekeo hadi ikajipeleka kujidhalilisha Butiama."

Mara kinokia chake kinalia. Anapokea simu na kuanza kuchonga. "Yes tuko huku Mikocheni kushuhudia upuuzi wa miujiza ya matapeli. Tumekimbia Kariakoo maana kuna furiko la vinyesi vya magabacholi pale. Kumbe wale watoto siyo misukule bali wabaini wanafiki. Mwenzangu nipe za Mwitongo."

Upande wa pili wa simu unachonga. "Huku mzee ni vituko. Bia zimepanda bei hata ngono. Vyangu wote wa kisiasa na kimaadili wamekusanyika hapa. naona kama umefika wakati wa makaburi ya watakatifu kufagiliwa na walevi, mafisadi,wezi na wazinzi. Hakuna cha muafaka wala serikali ya mseto Zenj? Sijui madevu atawambia nini CUF! Upo hapo msomi?"

Msomi anaendelea. "In principle yanayotokea ni ishara ya kuishiwa na kuharibikiwa. Leo hii tunaletewa majina mawili ya vidagaa wa EPA ilhali mapapa yakibakia maofisini kuharibu ushahidi. Juzi nilishangaa kusikia eti huyu Pinda pinda atawashughulikia ilhali wameishamzidi kete. Mbona hawawajibishi akina Hoseya na Mwananyika waliohusishwa moja kwa moja na Richmonduli? Mbona hawamuhoji Mkuu wala Nambari wani na kampuni lao la Deep Green Fisadi? Hivi nani anamdanganya nani hapa?"

kabla ya kuendelea, Mchunguliaji ananyaka mic. "Msomi naomba nikukosoe ila sikukosei adabu. Hivi mnamtaka Mkuu aeleze nini kuhusiana na EPA na Makanjanja ilhali ndiyo nyenzo zake za kuukwaa? Mie naona wamempa ulaji huyu mama tapeli wa kiroho wakidhani anadili ili awaombee wakati naye ni wa kuombewa. Mkuu kaishiwa kweli kweli. Hajui kuwa kuna makanjanja wa kisiasa, kitaaluma na waganga njaa sawa na madaktari wa mazingaombwe waliotamalaki Bongo? Nadhani hii ni Kaya pekee duniani ambapo majuha yanaweza kuwatangulia wajanja walioharibiwa na njaa ya kutengenezwa."

Msomi anamuunga mkono Mchunguliaji. "Mzee kwa mipwenti sina hamu. Hivi jana ulikunywa ulabu gani kiasi cha kuwa na mipwenti kama Mchonga nami?" Mchunguliaji anakenua kwa kupewa maujiko.

Msomi anaendelea. "Hivi mnadhani ni mchezo kwa watu walio hai kuishiwa hadi wakajificha nyuma ya umaarufu wa marehemu? Yesu alisema: waache wafu wazike wafu wenzao. Nami nasema wanakaya tuanze kupambana na kuachana na wafu wazikane iwe katika jina la chama au Yesu wanayemtumia kuubia umma wa wachovu wenye matatizo. Nimalizie na hili la makanjanja. Hivi ni kanjanja gani anamsema kanjanja gani. Kanjanja ni kanjanja. Awe wa kisiasa au kiroho na kiuandishi wote ni makanjanja. Huyu Rwakaterehe amethibitisha umbumbumbu na utapeli wake kwa jina la Yesu . AMINA."

Anakoha kidogo na kuendelea. "Nyie ngojeni muone aibu ya Butiama. Hakuna mzimu utakaowaua kama ule wa Richmonduli na BoT."

Akiwa anajiandaa kumwaga sera mara tuliona gari la mandata likiwapitisha wale watoto nasi tukatimka kuelekea kituo cha polisi.
Yaliyofuatia usiulize waulize CCM na CUF.

Source: Tanzania Daima Aprili 2, 2008

No comments: